TIC YASIKITISHWA NA HALI YA UWEKEZAJI KUPITIA KAMPUNI YA KATANI LIMITED, TANGA


Meneja wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Bw. Daudi Riganda kushoto akimsikiliza kwa umakini Kaimu Mkurugenzi wa kampuni ya Katani Limited ambaye pia ni Mkurugenzi wa fedha wakati wa ziara yao kwenye kampuni hiyo
Meneja wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Bw. Daudi Riganda kushoto akimsikiliza kwa umakini Kaimu Mkurugenzi wa kampuni ya Katani Limited ambaye pia ni Mkurugenzi wa fedha wakati wa ziara yao kwenye kampuni hiyo kulia ni Nestory Kissima


 Meneja wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Bw. Daudi Riganda kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa kampuni ya Katani Limited ambaye pia ni Mkurugenzi wa fedha na kushoto ni Nestory Kissima wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya mazungumzo hayo


 

NA MWANDISHI WETU,TANGA

 

Timu ya Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) ikiongozwa na meneja wake Bw. Daudi Riganda leo wametembelea Kampuni ya Katani Limited. 

Kampuni hii iliandikishwa na kupewa hadhi ya mwekezaji mahiri mwaka 2013, hata hivyo uwekezaji wake umekuwa ukisuasua kutokana na mgogoro mkubwa uliosababishwa na mkopo mkubwa uliokopwa na kampuni hii na baadaye kushindwa kulipwa kwa wakati. 


Hali hii imepelekea kampuni kuelekea kufilisika, kama sio kufa kabisa.Kampuni ya Katani Limited ilichukua mkopo wenye thamani ya Dola za Kimarekani milioni 10 kutoka NSSF kwa ajili ya kufanikisha uwekezaji kwenye zao la katani, kwa sharti kwamba NSSF wapewe hisa kwenye kampuni hii. NSSF wanamiliki asilimia 41 kwenye kampuni ya Katani Limited.

Hata hivyo, baada ya kushindwa kulipa mkopo huo kutoka NSSF wakulima walianza kulalamika kutokana na kushindwa kulipwa haki zao kwa wakati. Uwepo wamadeni mengi kutoka kwa wakulima wadogo waliokuwa wanazalisha mkonge na mkopo kuliathiri kwa kiasi kikubwa maendeleo ya mradi huu.

“Hadi kufika muda huu kampuni ya Katani Limited ilikuwa haijaanza kulima mkonge bali walichokuwa wanafanya ni kuingia mikataba na wakulima wadogo ambao ndio waliokuwa wanazalisha mkonge na kisha kuuuza kwenye kampuni ya Katani ambao waliuchakata na kutengeneza bidhaa mbalimbali zinatokana na mkonge”, alisema Bw. Riganda.

Alisema baada ya wakulima wadogo kulalamika kwa muda mrefu juu ya kutokulipwa kwa madeni yao na mapungufu mengine ikiwemo kutokulipwa kwa deni lililopo NSSF, kumechangia kampuni hiyo kuyumba ndipo mwaka 2019 wakurugenzi wa Katani Limited walikamatwa na kuifunguliwa kesi ya uhujumu uchumi, kesi ambayo inaendelea hadi hivi sasa. 

Kutokana nawakurugenziwa kampuni hii kuendelea kuwa mahabusu na mkurugenzi mtendaji wake kufariki akiwa mahabusu, kampuni hii imeyumba sana hali inayoonesha kufikia kikomo.

Bw. Riganda anatoa wito kwa wawekezaji mahiri na wengine kutumia mitaji yao kama ilivyokusudiwa na kutumia uwezo walionao katika kusimamia mitaji hiyo kwa faida yao, taifa na jamii kwa ujumla.

“Tumeona kampuni hii ilijitahidi kushirikisha wakulima wadogo lakini haikuweza kutimiza mpango wake kama ilivyokusudiwa baada ya kuingia kwenye mgogoro ambao hatimaye ulisababisha kampuni hii kufunguliwa kesi mbalimbali kutoka kwa wadau na washirika wake. Kwa vile kesi hii iko mahakamanitusingependa kuzungumzia sana suala hili”, alisema.

Akizungumzia kuhusu dhana ya wawekezaji mahiri kwa ujumla Bw. Riganda alisema hawa ni wawekezaji wakubwa na wenye mitaji mikubwa ambao sheria inawaruhusu kufaidi au kupata vivutio zaidi ya vile ambavyo vinatolewa kwa wawekezaji wa kawaida. 

Sheria inawataka wawekezaji mahiri ambao ni watanzania kuwa na mitaji ambayo haipungui Dola za Kimarekani milioni 20 kwenye uwekezaji watakaoufanya, na kwa wale raia wa kigeni wanatakiwa kuwamitaji ambayo haipungui Dola za Kimarekani milioni 50 kwenye uwekezaji watakaoufanya. 

Aidha, kuna wawekezaji mahiri maalum ambao mitaji yao inatakiwa isipungue Dola za Kimarekani milioni 300.

Bw. Riganda alisema taarifa walizopata kupitia kwa wawakilishi wa kampuni ya Katani ni kwamba hawakuwahi kufaidi vivutio vilivyopo kwenye mkataba walioingia na serikali kama wawekezaji mahiri kutokana na uelewa mdogo uliohusu vivutio hivyo.

Awali akizungumza wakati wa ziara hiyo Kaimu Mkurugenzi wa kampuni ya Katani Limited ambaye pia ni Mkurugenzi wa fedha alisema aliajiriwa mwaka 2012 baada ya kampuni ya Katani kuchukua mkopo wa pili kutoka NSSF. 

Alisema moja ya sharti ambalo lilikuwepo kwenye kwenye mkataba huoni kwamba ilitakiwa waajiri mkurugenzi mpya wa Fedha na ndipo yeye aliitwa kwenye usaili na kufanikiwa kupata nafasi hiyo. 

Wakati mkurugenzi huyu anaajiriwa aliwashauri namna ya kutumia fursa za uwekezaji vizuri, hata hivyo anakiri wamiliki wa kampuni walishindwa kutumia ipasavyo fursa hiyo ikiwa ni pamoja na vivutio vilivyotolewa kwenye mradi huo.

Baada ya mkopo wa NSSF kushindwa kulipwa, NSSF walikamata mali zote zilizokuwa zinamilikiwa na kampuni ya Katani Limited.

“Kampuni ya Katani ilikuwa inamiliki vifaa vya kusindika mkonge, korona na kiwanda cha kushona mazulia na kamba vilivyopo Ngombeni Muheza lakini tulikuwa na mkataba na wakulima wa kugawana mapato baada ya mkulima kuleta mkonge akishapata singa katani anauza na anarudi kumlipa mkulima stahili yake”, alisema

Katika kipindi cha mwaka 2012 na 2013 kampuni hiyo ilifanikiwa kutengeneza faida kidogo lakini kama biashara kukawa kuna ucheleweshwaji wa kuwalipa wakulima wadogo. Alisema hali hiyo ndio ilileta mgogoro baina ya wakulima wadogo naKatani Limited

Alisema ilipofikia mwezi Oktoba mwaka 2019 kulikuwa na Mkutano wa Mkuu wa Mkoa na mkutano huo uliwapeleka ndani watu wote wa Bodi ya Wakurugenzi wa Katani na hiyo ilitokana na mkaguzi wa serikali ambaye alitumwa kufanya ukaguzi na alipowasilisha taarifa yake ndipo RC aliagiza wakamatwe na yeye alifanikiwa kutoka Oktoba 31 mwaka huo.


Alisema baada ya kutoka alibidi alazimike kukaimu nafasi hiyo na NSSF tayari walishafungua kesi mahakamani. Hivi sasa kuna zoezi linafanyika la mthamini wa mali kuhakiki na mali zote za kampuni ya Katani ili kuona kama thamani yake itatosha kufidia deni lililokopwa na kampuni hiyo au la.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments