MAFUNDI CHEREHANI WAUAWA KWA KUPIGWA MARUNGU KISHA KUCHOMWA MOTO SHINYANGA

Watu watatu wanaodaiwa kuwa ni mafundi cherehani wakazi wa kijiji cha Kizungu kata ya Lyamidati tarafa ya Nindo wilaya ya Shinyanga wameuawa kwa kupigwa marungu na wananchi wa kijiji hicho baada ya kubainika kuwa wamemdanganya kamanda wa jeshi la jadi sungusungu kwamba wameibiwa vitambaa vya kushona pamoja na nguo.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka jeshi la polisi mkoa wa shinyanga tukio hilo limetokea juzi majira ya saa nne usiku,ambapo mafundi cherehani hao watatu waliuawa kwa kupigwa marungu sehemu mbalimbali za miili yao na kisha kuchomwa moto na wananchi waliojichukulia sheria mkononi.
Kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga kamishina msaidizi wa polisi Evarist Mangalla aliwaja watu waliouawa kuwa ni Juma Silivester(27),Ruben Silivester(30) na Juma Marco(26) wote ni mafundi cherehani wakazi wa kijiji hicho cha Kizungu.
Kamanda Mangalla alieleza chanzo cha mauaji kinatokana na wananchi kujichukulia sheria mkononi baada ya mafundi  cherehani hao kubainika kuwa walitoa taarifa za uongo kwa kamanda wa sungusungu kwamba wameibiwa vitambaa mbalimbali vya kushona pamoja na nguo kwenye kibanda chao cha kushonea ambapo baada ya ufuatiliaji wa taarifa hizo walibaini kuwa vitu hivyo vilikuwa katika nyumba za wahusika.
Aliongeza kuwa  kitendo hicho kiliwakera wananchi na kuanza kuwapiga marungu na kisha kuwachoma moto watu hao.
Kamanda Mangalla  alisema juhudi zakuwasaka na kuwakamata watu waliohusika na mauaji hayo bado zinaendelea huku akiwataka wananchi kutoa taarifa zitakazosaidia kukamatwa kwa wahusika hao kwani kitendo hicho ni ukiukwaji wa haki za binadamu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post