LEMBELI ASEMA SERIKALI YA CCM INAELEKEA KUBAYA KUFUNGIA MAGAZETI


Mbunge wa Kahama, James Lembeli

Wakati Mbunge wa Kahama, James Lembeli (CCM), akisema kuwa serikali yoyote yenye dalili za kuelekea kubaya huanza kufungia au kudhuru vyombo vya habari halafu binadamu, Muungano wa Mabaza ya Habari Duniani (WAPC) na Shirikisho la Kimataifa la Waandishi wa Habari (IFJ) wamelaani kitendo hicho.
Kauli hizo zimekuja zikiwa zimepita siku chache tangu serikali kuyafungia magazeti ya Mwananchi kwa siku 14 na Mtanzania siku 90, kwa kile kinachodaiwa ni kuchapisha habari za uchochezi.
Lembeli ambaye kitaaluma ni mwandishi, alisema kuwa serikali yoyote inayotumia mabavu kama hayo, hapo kuna madhara, na kwamba ni dalili mbaya kwamba inakoelekea siko.
Alisema kuwa amesikitishwa na hatua hiyo ya serikali kuyafungia magazeti hayo kwa kutumia sheria kandamizi ya magazeti ya mwaka 1976, wakati vyombo vya habari siku zote ndivyo vimekuwa watetezi wa wanyonge.
Lembeli alifafanua kuwa sababu kama hizo wakati mwingine ndizo zinawafanya wananchi kukosa imani na serikali yao, hivyo hata wanahabari wanapodhuriwa wanaihusisha serikali na matukio hayo.
Alisema kuwa kufungia vyombo vya habari si suluhisho la kutofichua maovu, kwani siku hizi nchi ipo katika teknolojia ya kisasa na kwamba ukifungia gazeti wanatumia mitandao.
“Ukifungia mitandao ya online, wanatumia kuhabarishana kwa njia za simu. Ukianza kumuona baba anaziba midomo ya mtoto wake anayehoji na kudadisi, basi hiyo nyumba ni lazima iwe na matatizo.
“Suluhisho hapo ni kujibu hoja na si kufungia, na kama kuna kosa, basi baba anatakiwa kuwa wa kwanza kumkanya mtoto kwa njia sahihi badala ya kufunga mdomo,” alisema.
Kwa mujibu wa Lembeli, sheria ya magazeti ya mwaka 1976, imepitwa na wakati huku akishangaa sababu za serikali kushindwa kupeleka muswada bungeni kuifanyia marekebisho.

CHANZO;TANZANIA DAIMA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post