MGEJA AMPANDILIA SUMAYE-AMSHAURI AACHE PAPARA

Hamis Mgeja

Mwenyekiti wa taasisi ya Tanzania Mzalendo Foundation nchini, Khamis Mgeja amepinga kauli iliyotolewa na waziri mkuu mstaafu, Fredrick Sumaye akidai kumuunga mkono Rais Jakaya Kikwete katika vita dhidi ya rushwa nchini na kwa lengo la kuonesha ni miongoni mwa watu wanaochukizwa na vitendo hivyo.
Akizungumza na waandishi wa habari juzi kijijini kwake Nyanhembe kata ya Kilago wilayani Kahama mkoani Shinyanga, mwenyekiti huyo ambaye taasisi yake inashughulika na masuala ya utawala bora, utamaduni, michezo na haki za binadamu alielezea kushangazwa kwake na kauli hiyo na kueleza siyo kweli Sumaye anaichukia rushwa kama alivyodai kwa vile wakati akiwa waziri mkuu ariruhusu kufanyika mambo mengi yaliyokuwa yakiashiria mianya ya rushwa.

Alisema katika kipindi hicho, Tanzania ndipo ilipofunga mikataba mingi mibovu katika sekta ya madini, viwanda, mashamba na ranchi za taifa ikiwemo uuzwaji wa benki ya umma (NBC) iliyouzwa kwa bei ya kutupa ikiwa ni mikataba iliyofungwa kutokana na rushwa kubwa.
“Binafsi napingana na Sumaye katika hili, siyo kweli anachukizwa na tatizo la rushwa hapa nchini kama kweli angekuwa na sifa hiyo basi wakati wa kipindi cha uongozi wake asingeruhusu nchi yetu kufunga mikataba mibovu, leo hii watanzania wanalia kwa mikataba mibovu iliyofungwa wakati wake,”alisema Mgeja
“Katika kipindi chake rushwa ilikuwa kubwa sana, hata rushwa ya ngono ilishamiri wakati huo ili mtu aweze kupata ajira, kama anabisha mimi nitamtajia watu waliopewa ajira wake wake baada ya kutoa rushwa ya ngono, leo hii usafi anaodai anao uko wapi,”aliongeza
“Mimi nampa ushauri wa bure ni vizuri aache kupaparika akae chini atulie, maana kauli zake anazozitoa hivi sasa anaonekana amekuwa ni mtu wa kulalamika kila siku, hatoi ushauri nini kifanyike ili tufikie mafanikio, asiwakumbushe watu vidonda alivyowasababishia wakati wa uongozi wake,” alieleza Mgeja.
Mgeja alielezea kushangazwa kwake ni kitendo cha vyombo vya dola kuendelea kufukuzana na vidagaa huku vikiwaacha mapapa waliosababisha nchi kuingia katika matatizo makubwa ikiwemo wizi wa fedha za EPA, Meremeta, mikataba ya Songas na IPTL ambayo yote yalifanyika wakati wa Sumaye.
“Tunashangaa hii nguvu ya kuwasonta vidole wenzake anaipata wapi au ana lengo la kufunika madhambi yake aliyoyafanya wakati akiwa waziri mkuu, lakini suala la rushwa analopigia kelele hakuna mtanzania anayelipinga wote tunakerwa na rushwa, ni vizuri angeonesha mfano mzuri kwa kukemea mikataba mibovu iliyofungwa katika kipindi chake,” alisema Mgeja.
Alisema uingiaji wa mikataba mibovu inayoiumiza nchi hivi sasa ni rushwa kubwa kushinda rushwa ndogondogo anazozipigia kelele Sumaye na kwamba huenda kinachosababisha apige kelele na kutapatapa ni baada ya kuangushwa kwenye uchaguzi wa mjumbe wa NEC wilayani Hanang mkoani Manyara ambako alishindwa na Mary Nagu.
Pia Mgeja alitoa mfano wa maamuzi mabovu yaliyofanyika kipindi cha uongozi wa Sumaye kwa kuamua kuuza nyumba za umma zilizojengwa kwa nguvu ya watanzania wote wakiwemo wafugaji, wavuvi na wakulima ambao hawakushirikishwa katika kufikia maamuzi ya kuuzwa kwake na badala yake waliokumbuka ni wafanyakazi peke yao.
Akijibu swali kutoka kwa waandishi wa habari iwapo hivi sasa yupo katika harakati za kumfanyia kampeni mmoja wa watu wanaotaka kuwania urais nchini, Mgeja alisema yeye binafsi haamini kama ni wakati muafaka wa watanzania kuanza kulumbana juu ya mtu gani awe Rais mwaka 2015.
“Mimi nafikiri suala nani awe rais mwaka 2015 siyo wakati wakati hivi sasa, na halipaswi kupewa nafasi ya kusababisha watanzania tugawanyike, tujengeane uhasama, chuki na fitina na kusababisha kupoteza umoja na mshikamano wetu tulionao, maana urais unapangwa na mungu mwenyewe yeye ndiye anayemjua rais ajaye atakuwa nani,” alisema Mgeja.
Alisema suala la rais ajaye tayari limo ndani ya mioyo ya watanzania, ndiyo wanaojua ni nani atakuwa rais wao baada ya Rais Kikwete,  hakuna sababu ya kulumbana na kwamba iwapo kelele za Sumaye ni juu ya kutaka kuwania urais mwaka 2015, ni vizuri akawaachia wananchi wenyewe ndiyo wataamua wakati utakapofika.
“Kama kelele hizi za mwenzetu ni urais wa mwaka 2015, tunamshauri aache kupaparika, akae chini atulie, na asiwasonte vidole vibaya wenzake, hakuna mtantania mwenye hatimiliki ya urais hapa nchini, wote wana haki sawa, ni juu ya watanzania wenyewe kuamua rais wao awe nani,” alisema Mgeja.
Hata hivyo alisema ni vizuri rais ajaye awe na sifa mbili kuu moja ni kuwekeza hisa za imani kwa watanzania, anayeaminika na sifa ya ziada iwe ni uwezo wa kutatua changamoto zilizopo nchini.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post