RONALDO APIGA BAO LA HATARI REAL MADRID IKITOKA SARE YA 2-2 DHIDI YA VALENCIA

article-2620071-1D9363A900000578-742_634x463SOKA kama unalijulia raha sana!. Mwanasoka bora wa dunia, Mreno Cristiano dos Santos Aveiro Ronaldo jana ameiamsha dunia tena baada ya kupiga bao moja tamu mno na kuinusuru Real Madrid kuzama dhidi ya Valencia.

Mechi hiyo ya kukata na shoka ilimalizika kwa timu hizo mbili kutoka sare ya mabao 2-2.
Valencia almanusura ibebe pointi zote tatu Uwanja wa Santiago Bernabeu, lakini Ronaldo dakika ya 92 aliinusuru timu yake tena kwa kufunga bao baada ya kuunganisha kwa utaalum wa hali ya juu krosi murua iliyochongwa na Angel di Maria.

Mathieu alianza kuifungia Valencia dakika ya 44, lakini Sergio Ramos akaisawazishia Real Madrid dakika ya 59 na Parejo akawafungia wageni bao la pili, kabla ya Ronaldo kufunga bao lake la 50 msimu huu. 

Atletico Madrid na Diego Costa wake jana wamechapwa 2-0 na Levante, lakini bado wanaendelea kuwepo kileleni mwa La Liga kwa pointi zake 88 za mechi 36, ikifuatiwa na Barcelona pointi 85 mechi 36 wakati Real sasa ni ya tatu kwa pointi zake 83 za mechi 35. 

Baada ya mechi hiyo, kocha wa Real Madrid Carlo Ancelotti anaamini bao la dakika za majeruhi la Ronaldo limeendelea kuwaweka katika mbio za ubingwa.

Madrid sasa wapo nyuma kwa pointi tano na Vinara Atletico, huku wakiwa na mchezo mkononi, na Ancelotti raia wa Italia anaamini kuwa asingekuwa Ronaldo miamba hiyo ya soka la Hispania ingejiondoka katika mbio za ubingwa.

“Goli la Ronaldo ni muhimu sana kwasababu kupoteza mechi ingemaanisha tumepoteza ubingwa”. Ancelotti aliwaambia waandishi wa habari.

“Kama nilivyosema hapo mwanzo, ubingwa utaamuriwa kwa mechi ya mwisho. Imekuwa wiki ngumu kwa timu zote tatu za juu”.

“Timu ilianza mchezo vizuri lakini ilikuwa ngumu kwetu kwasababu tulishindwa kuendelea na kasi ile. Tulipoteza nafasi nzuri za kufunga, lakini bado nafasi ya ubingwa ipo”.
Licha ya matukio haya katika mechi za La Liga, suala  la ubaguzi wa rangi limezidi kuitikisa Hispania baada ya mchezaji wa Levante, Pape Diop kuzomewa na kufanyiwa ishara za nyani jana na mashabiki wa Atletico Madrid wakati wa mechi ya La Liga. 

Hii ni wiki moja baada ya beki wa Barcelona, Dani Alves alipolazimika kula ndizi aliyotupiwa na mashabiki uwanjani wakati akijiandaa kupiga mpira wa kona. 

Kiungo huyo raia wa Senegal baada ya mechi alisema alicheza kama nyani mbele ya waliomzomea na kumkebehi.
“Waliniita nyani,niligeukia na kujifanya nyani,Nimechoka na ubaguzi katika soka. Na upo mwingi”.” Diop alikaririwa na Marca.com.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
أحدث أقدم