ASKOFU AWALIPUA TENA WABUNGE WA SHINYANGA MJINI NA KISHAPU,AIONYA CCM

Askofu Edson Mwombeki katika picha ya pamoja na mbunge wa Jimbo la Shinyanga mjini, Stephen Masele pamoja na mmoja wa vikongwe wanaotunzwa na kanisa la Tanzania Field Evangelism Shinyanga.


ASKOFU wa kanisa la Tanzania Field Evangelism la mjini Shinyanga, Edson Mwombeki amekitahadharisha Chama cha Mapinduzi (CCM) huenda kikajikuta katika wakati mgumu kwenye uchaguzi mkuu ujao kisipokemea tabia ya wabunge wake wanaotoa ahadi kwa wananchi bila ya kuzitekeleza.
 
Askofu Mwombeki alitoa tahadhari hiyo ofisini kwake ambapo alisema CCM inaweza kujikuta ikipoteza majimbo ya Shinyanga mjini na Kishapu iwapo haitawaweka kitako wabunge wake, Stephen Masele na Suleiman Nchambi kwa lengo la kuwahimiza ili watekeleze ahadi zao kwa wananchi.
 
Mbali ya tahadhari hiyo Askofu Mwombeki alisema kanisa lake halitokuwa tayari kumpigia kampeni mbunge ye yote atakayeshindwa kutekeleza ahadi zake na kusimamia vyema ilani ya uchaguzi ya chama chake huku akijipanga kurudi kugombea tena ubunge akitegemea kutumia fedha kuwarubuni wapiga kura.
 
Alisema iwapo CCM itashindwa kuwarekebisha wabunge hao kwa kuhakikisha wanatimiza ahadi walizozitoa kwa wananchi kanisa lake litasimama kidete kuwahimiza wananchi katika majimbo yao wasiwachague tena kwa vile watakuwa wameonesha wazi kugombea kwao awali haikuwa kwa ajili ya maslahi ya wananchi bali kutafuta maslahi yao binafsi.
 
Akimzungumzia mbunge wa jimbo la Shinyanga mjini Askofu huyo alisema mara baada ya kuchaguliwa kuwa mbunge wa jimbo hilo alitoa ahadi nyingi ambazo kwa sehemu kubwa ameshindwa kuzitekeleza ambapo amediriki hata kulidanganya kanisa kitu ambacho hakina sura nzuri mbele za mungu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post