ASKOFU MWOMBEKI AWALIPUA WANAOJITANGAZA KUWANIA URAIS,ADAI HAWANA SIFA HATA MAJIMBO YAO YA UBUNGE YAMEWASHINDA


Askofu wa kanisa la Tanzania Field Evangelism(TFE) maarufu kanisa la Emmanuel la mjini Shinyanga Edson Mwombeki

Watanzania wametakiwa kuwa makini na watu wanaoibuka kila kukicha wakijitangaza kuwania nafasi ya urais ili waende ikulu kwani baadhi yao hawana sifa ya kuwania nafasi hiyo na wengi wao hawafanya lolote la maana hata kwenye majimbo yao wananchi wanaendelea kuwa na maisha magumu kila kukicha.

Hayo yamesemwa na Askofu wa kanisa la Tanzania Field Evangelism(TFE) maarufu kanisa la Emmanuel la mjini Shinyanga Edson Mwombeki wakati wa kuhitimisha siku tatu kavu za maombi pasipo kula wala kunywa yaliyofanywa na wachungaji 40 kutoka mkoa wa Shinyanga lengo likiwa ni kuombea taifa amani ikiwemo kumwomba mungu aliepushe taifa na watu ambao mungu hajakusudia wagombee urais.

Askofu Mwombeki alisema hivi sasa kuna wimbi la kila mtu kujitangaza kuwania urais ili waende ikulu lakini baadhi yao hawana sifa hiyo hata majimbo yao yamewashinda ,wameshindwa kuwaletea maendeleo wapiga kura wao.

Alisema nafasi ya urais ni nyeti sana hivyo haiwezi kuchezewa na kila mtu hivyo kuwataka watanzania kuwa makini na watu hao wasije kuliingiza taifa kwenye matatizo ikiwemo kupoteza amani iliyopo sasa.

“Kati ya waliotangaza nia ya kuwania urais wapo wenye sifa,lakini kuna wengine hata majimbo yao yamewashinda,wengine wanadiriki kutumia pesa zao kusaka urais,wengine kukimbilia kwa waganga wa jadi wakiamini nguvu za giza zitawapatia nafasi za uongozi,hii ni hatari sana,tusipokuwa makini taifa litaangamia”,alieleza Mwombeki.

Askofu Mwombeki alisema watu wengi wakati wa uchaguzi wamekuwa wakitumia pesa zao na nguvu za giza kusaka uongozi na kuongeza kuwa katika uchaguzi wa mwaka huu watashindwa kwa nguvu ya mungu na nguvu ya wananchi(umma).

“Tunahitaji rais mzalendo na nchi yake mwenye hofu ya mungu  bila kujali anatoka chama gani cha siasa,atakayesimamia maslahi ya nchi , kusimamia rasilimali za nchi badala ya anayetumia nafasi ya uongozi wake kujinufaisha mwenyewe,tunawashangaa wanaolilia ikulu,sijui wanafuata nini huko,maana hata Hayati Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kusema mtu anayelilia kwenda ikulu siyo mzuri,anapaswa kuangaliwa kwa makini”,alieleza askofu Mwombeki.

Askofu huyo alikitaka Chama Cha Mapinduzi kuwa makini na wagombea wake na kisipokuwa makini kuweka kiongozi mzuri  vinginevyo taifa linaweza kupata rais atakayelipeleka taifa pabaya.

Hata hivyo mbali na kusema wapo watu wenye sifa ya kuongoza nchi ya Tanzania,askofu huyo hakutaja majina yao na kuahidi kutaja majina yao mwezi Februari mwaka huu wakati wa mkutano wa maombi wa maaskofu na wachungaji kutoka kanda ya ziwa Victoria.

Askofu Mwombeki aliwaomba viongozi wenzake wa dini kufanya maombi ya dhati kuiombea nchi amani hasa katika kipindi hiki ambacho taifa linaelekea kufanya matukio makubwa mawili ya kupigia kura katiba pendekezwa na uchaguzi mkuu.

“Yapo matukio makubwa mawili yatafanyika hapa nchini,suala la katiba na uchaguzi lakini tayari kuna dalili mbaya zinajionesha,sasa hivi kuna kundi la wahalifu “Panya Road” linayumbisha nchi,tunapaswa kuwa makini sana kwani nidhamu ya nchi imeanza kupotea”,aliongeza Askofu Mwombeki.

Katika hatua nyingine aliwataka watanzania kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika daftari la wapiga kura kwani ndiyo sehemu pekee watakayoitumia kupata viongozi wanaowataka katika uchaguzi mkuu ujao.
Na Kadama Malunde-Shinyanga

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post