Mwendesha
pikipiki aitwaye Jackson Alfred(22) mkazi wa Ngalama-Kakonko mkoani
Kigoma na abiria wake Kashindye James(6) ambaye ni mtoto wa kike wamefariki dunia mjini
Kahama, baada ya pikipiki waliyokuwa wamepanda kugongwa na lori.
Kwa
mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na kamanda wa polisi mkoa wa
Shinyanga Justus Kamugisha, tukio hilo limetokea jana mchana katika
kijiji cha Igomelo kata Malunga, wilayani Kahama.
Amesema
gari lenye namba T679 AUN aina ya Mitsubishi Fuso Tiper mali ya Issa
Obeid Mkwale mkazi wa Ngara ikiendeshwa na Athuman Juma(35) mkazi wa
Nyakato-Kahama iligonga pikipiki hiyo yenye namba za usajili MC.993ACX
aina ya Sunlg.
Kamanda
Kamugisha amesema Jackson Alfred alifariki dunia papo hapo, huku mtoto Kashindye James ambaye
alikuwa abiria akifariki dunia jana saa 12 jioni wakati akipatiwa
matibabu katika hospitali ya wilaya ya Kahama.
Hata
hivyo Kamanda Kamugisha amesema jeshi la polisi linafanya uchunguzi wa
chanzo cha ajali hiyo na kuongeza kuwa dereva wa gari hilo anashikiliwa
na polisi kwa hatua zaidi za kisheria.
|