Duh!! ASKARI POLISI AWACHARANGA MAPANGA MAMA NA MTOTO KISA ANAWADAI CHUPA 2 TUPU ZA BIA

 
Polisi  aliyetimuliwa kazi, Godfrey Mushumbusi (42), amewakata mapanga na kuwajeruhi mama na mwanae kisa anawadai chupa mbili tupu za bia.

Sekela Mwiniwasa (44) na mtoto wake Ricado Dancan (24), mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,  walikatwa mapanga na kupigwa virungu maeneo tofauti mwilini wakiwa kwenye  baa ya Itawa inayomilikiwa na  askari huyo Alhamisi wiki hii.

Mkasa huo uliotokea  Tabata Kisukuru, ulithibitishwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ilala, Marietha Minangi na kusema kwamba chanzo ni familia hiyo kushindwa kupeleka chupa hizo kwa wakati na kulipa deni la Shilingi 10,000. 

Alisema mtuhumiwa alifikishwa kituoni na kuachiwa kwa dhamana na upelelezi unaendelea kabla ya kufikishwa mahakamani.

 Akisimulia mkasa huo, Sekela alisema Jumanne ya wiki hii alimwagiza mdogo wake, Leah Mwaipaja bia mbili  kwenye baa hiyo na siku iliyofuata Mwaipaja alivyopita kwenye baa  hiyo, mmoja wa wahudumu wake  Sophia akamuuliza  mbona hajarudisha chupa. 

“Alimjibu ziko  kwenye mfuko lakini  amezisahau na kuahidi kuzipeleka,” alisema na kuongeza kuwa Sophia alianza kumporomoshea matusi ya nguoni kitendo kilichomsababisha arudi nyumbani na kumueleza mke wa Msumbushi aliyekuwa nyuma ya baa  hiyo.

Alieleza kuwa  wakati anarudi nyumbani, mhudumu huyo  alimfuata na kumweleza kwa nini alitoa taarifa hizo kwa bosi wake na kuanza kumshambulia.

“Walipigana mbele ya baa hiyo na mke wa mtuhumiwa alikuwapo na kuwachochea kwa maneno ili ugomvi uendelee, lakini aliona haitoshi akachukua fimbo kumtandika nayo,” alisema.

Baada ya kipigo Mwaipaja alirudi nyumbani na kuelezea kichompata hivyo Sekela akalazimika kwenda naye  kumaliza  tatizo hilo lakini alijibiwa vibaya na Sophia na kuondoka.

“Nikiwa kwenye  eneo hilo, mume wangu alipita  akitokea kazini nilimsimulia  kilichotokea kabla sijarudisha chupa hizo.

Baada ya kuzikabidhi nilianza kutukanwa na wahudumu matusi ya nguoni ambayo yalishuhudiwa na watoto wangu akiwamo aliyejeruhiwa,” alisema na kuongeza:

“Ricado alimshika mmoja wa wahudumu na kumuuliza kwa nini ananitukana, ndipo polisi huyo akanishika na kunipiga rungu  kichwani hadi nikazirai  na kisha kumkata mtoto wangu mapanga  mikononi,” alisema.

Alisema askari huyo baada ya kuona amewajeruhi, alimwagiza mlinzi  aliyekuwapo eneo hilo atoe mshale  atumalizie lakini naye  alikataa , wakati akiwakata mapanga aliwatishia kuwa kila  jeraha watalazimika kulilipia  kwa riba.

“Ninachokumbuka niliona watu wamejaa eneo la tukio na baadaye nilizirai nilipoamka nilikuwa  hospitali ya Amana,  nimeshonwa nyuzi saba kichwani na mwili wote unauma,” alisema.

Alisema baada ya tukio hilo, mtuhumiwa alipiga simu polisi na kudai amevamiwa na  panya road ambapo gari la polisi lilifika lakini kutokana na maelezo yake kupishana, polisi walifanya uchunguzi na kubaini kuwa aliwadanganya.


“Alikutwa na mkewe wakiwa wamelowa damu, polisi waliwauliza hao panya road wamekujeruhi wapi, akadai walifika na kuanza kukatana mapanga wenyewe kwa wenyewe, wakakimbia, lakini mama mmoja aliyekuwepo eneo la tukio  aliwaeleza ukweli wa mambo ndipo Msumbushi akapelekwa kituo cha polisi Stakishari,” alisema.

Na Romana Mallya-NIPASHE JUMAPILI

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post