MAASKOFU NA WACHUNGAJI 200 WALILIA KATIBA MKESHA WA MWAKA MPYA 2015 MJINI SHINYANGA


Maaskofu na wachungaji wamesema huenda mchakakato wa kupata katiba mpya nchini ukakwama kutokana na kile kilichoelezwa kuwa maaskofu na wachungaji wachache sana wana nakala za katiba inayopendekezwa hali ambayo inawafanya wengi wao washindwe kuifafanua kwa usahihi mbele ya waumini wao.


Hayo yamesemwa na askofu wa kanisa la Tanzania Field Evangalism (TFE) la mjini Shinyanga Edson Mwombeki wakati wa ibada ya mkesha wa mwaka mpya 2015 iliyoenda sambamba na kufunga kongamano la siku 5 la wachungaji na maaskofu 200 kutoka mikoa mbalimbali nchini lenye lengo la kuombea taifa na kudumisha umoja katikati ya watumishi wa mungu.

Askofu Mwombeki alisema wachungaji na maaskofu wengi walioko katika wilaya na mikoa mbalimbali nchini hawana katiba inayopendekezwa kwa ajiri ya kupigiwa kura na wananchi mpaka sasa hali ambayo inazua hofu kwani wanashindwa kuifafanua kwa wananchi na badala yake wanasiasa ndiyo wamekuwa wakifafanua mambo ya katiba na kila mmoja akizungumzia kivyake.

“Huwezi kupigia kura kitu usichokielewa,maaskofu na wachungaji wameniambia wanataka katiba,waweze kuzungumza na watu wao kitu sahihi,kwani hivi sasa kila mwanasiasa anazungumza vya kwake,sisi tufanyeje sasa,hatutaki serikali ifike kipindi cha kupiga kura halafu watu wapige ndiyo au hapana wakati hawajaelewa,je wakipiga hapana wakati ilikuwa nzuri tutafanyeje?”alihoji Mwombeki.

Alisema lengo lao siyo kukataa katiba wala kupigizana kelele na serikali bali ni kusaidia kupatikana kwa katiba bora kutokana na serikali kutumia gharama kubwa,na kama gharama imetumika basi serikali ione umuhimu wa kugawa katiba pendekezwa bure.

“Tunapenda kumpongeza rais Kikwete kwa jitihada zake nzuri za kuonesha demokrasia iliyo imara katika taifa la Tanzania ikiwa na lengo la kuifanya nchi iendelee kuwa na amani,jambo ambalo amelifanya kwa bidii na nguvu zake zote na kufikia hatua ya kupata katiba pendekezwa ambayo sasa imefika hatua ya pili”,alieleza Mwombeki.


“Tunaomba rais Jakaya Kikwete atuamini,kama tusingeiombea wangepigana Dodoma,kinachotuuma sisi wachungaji tulilala makanisani tukiomba tukatuma wajumbe huko Dodoma hadi kufikia rais anaiinua katiba na kusema ni nzuri,sasa asije akatudharau,tunataka atuletee ili tujue mapema kama ni ya kuweka pembeni au la!,wanasiasa wanasema ni mbovu,sisi tufanyeje,tuwaambiaje watu wetu”,aliongeza Askofu Mwombeki.


Kwa upande wake Mchungaji Valentine Martine kutoka Missionary Pentecoste  Church Karagwe mkoani Kagera alisema hivi sasa wanashindwa kuelewa nini cha kuelimisha kwa wananchi kutokana na kutoelewa kichomo kwenye katiba hiyo hivyo wanahitaji wapewe katiba inayopendekezwa bure.

“Kila mwanasiasa anaongea lake,lakini jamii inatuamini sisi watumishi wa mungu,tukiisoma tukaielewa tutaipeleka kwa watu,sisi siyo wanasiasa, tutasema yaliyo kweli bila kuipindisha wala uongo,wasomi wanasema mwanasiasa mara nyingi wanaongea uongo,ukijua kweli utakuwa huru”,alisema mchungaji Martine.

 Naye mchungaji George  Daniel kutoka kanisa la Pentecoste Assemblies of God Tanzania(PAGT) Bariadi mkoani Simiyu alieleza kuwa anapata wasiwasi kusema katiba pendekezwa inafaa au la kutokana na kutojua katiba hiyo ina manufaa kwa jamii au la.
Na Kadama Malunde-Shinyanga

Bonyeza hapa Tukupe habari zote mara moja zikitoka "HABARI" VITUKO "MAPENZI"MAGAZETI,UDAKU>
Endapo una Habari,Picha,Video,Tangazo au Tatizo Lolote wasiliana nasi kwa namba  +255 688 405 951

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post