Mwanaume
mmoja anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 25 amekutwa akiwa amefariki
dunia maeneo ya Stanley Road Katika Manispaa ya Kigoma-Ujiji huku akiwa
hana nguo.
Akitoa taarifa hiyo kwa waandhishi wa habari hapo jana, Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Kamishina Msaidizi ACP Japhari
Muhamed, alisema kuwa mwili huo uliokotwa jana majira ya saa 1:00
asubuhi baada ya wananchi kuuona na kutoa taarifa Polisi.
Kamanda
alisema kuwa chanzo cha kifo hicho hakijafahamika hata jina lake
halijafahamika na wala ndugu zake hivyo mwili umehifadhiwa mochwari ili
kusubiri kama kuna ndugu atakaye jitokeza.
“Hata
hivyo jana marehemu alionekana mtaani akitembea uchi kama mtu mwenye
matatizo ya akili, uchunguzi wa tukio hilo bado unaendelea” alisema
kamanda.
Wakati
huohuo, Gereminye Kigonza mkazi wa kijiji cha Kazilamiunda kata ya
Kasanda Zone 22 Wilaya ya Kakonko mkoa wa Kigoma amefariki dunia baada
ya kupigwa na radi iliyosababishwa na mvuo kubwa iliyokuwa ikinyesha.
Kamanda alisema kuwa tukio hilo lilitokea mapema wiki hii majira ya saa 10 jioni wakati mvua kubwa ikinyesha.
“Kwa kipindi hiki mkoa huu umekuwa na mvua nyingi ambazo zinaambatana na radi ambazo zimekuwa zikileta madhara” alisema Kamanda.
Hata
hivyo Kamanda aliwataka wananchi kutokaa katika maeneo hatarishi wakati
wa mvua na kuwa waangalifu kwa matumizi ya vifaa vinavyotumia umeme
wakati wa mvua za radi.
Chanzo...E.Senny