Kaimu Meneja wa vipimo mkoa wa Shinyanga Nyagabona Mkanjabi akiwa amebeba mfuko ambao uzito wake hauendani na uzito ulioandikwa juu ya mfuko-picha na Marco Maduhu-Shinyanga |
Mfanyakazi wa kiwanda cha nafaka Gradi Super Sembe akipima nafaka kwa kutumia mizani ya kuazima-picha na Marco Maduhu-Shinyanga |
Ofisi ya wakala wa vipimo mkoani Shinyanga,
imekizuia kiwanda cha nafaka cha Gradi Super Sembe kinachofanya shughuli zake
mjini Shinyanga kuacha kutoa huduma yake kwa wananchi kwa muda, kutokana na
mizani zake kutokuwa sahihi ambazo zimechezewa kwa lengo la kuwaibia wateja
wanaonunua bidhaa za kiwanda hicho.
Tamko hilo limetolewa juzi na kaimu Meneja wa
vipimo mkoani humo, Nyagabona Mkanjabi wakati akizungumza na waandishi wa
habari ofisini kwake, kufuatia ukaguzi wa vipimo walioufanya kwenye viwanda vya
nafaka mjini Shinyanga na kukibaini kiwanda cha Gradi Super Sembe mizani zake
kuwa zimechezewa.
Mkanjabi alisema wakiwa kwenye ukaguzi huo wa
vipimo, walipofika kwenye kiwanda hicho cha nafaka na kuzikagua mizani
walibaini kuwa vipimo vyao havipo sahihi na wamekuwa wakiwaibia wananchi kwa
kuwapunja kilo, na kuamua kukisimamisha kutoa huduma kwa muda.
“Tulipofika kwanza kwenye kiwanda hicho kukagua
mizani zao, walituzuia tena ukawa ugomvi mkubwa, lakini kutokana na mujibu wa sheria,
walikubali kupima ambapo tulibani kuwa vipimo vyao havipo sahihi wamekuwa
wakifanya wizi mkubwa kwa wateja wanaonunua bidhaa zao”, alisema Mkanjabi.
“Ukiangalia mfuko wa unga wa sembe uliokwisha
fungwa umeandikwa una kilo 5, lakini ukiupima mfuko huo una kilo 4, kamili, na
pia tulijaribu kupita kwenye maduka wanaowauzia wateja wao na kutoa huduma kwa
wananchi, tukabaini madudu yale yale, tulichokifanya tumezuia kiwanda hicho
mpaka pale taratibu za kisheria zikakapofuatwa”,aliongeza.
Kwa upande wake mkurugenzi wa kiwanda hicho cha
nafaka Gradi Super Sembe, Dickson Msula, alikiri mizani zake kuchukuliwa na
wakala huyo wa vipimo kwa madai kuwa zimechezewa, huku akikanusha kuwa bidhaa
zake zipo kwenye vipimo sahihi na hazina upungufu wowote.
Hata hivyo Msula alisema agizo lililotolewa na
wakala huyo la kusitishwa kiwanda chake kutoa huduma kwa muda, hakubaliani
nalo, licha ya kuchukuliwa mizani zake ambapo ataazima mizani kwa viwanda
jirani ili kuendelea na shughuli zake, kwa kuhofia kupata hasara zaidi.
Na Marco Maduhu-Malunde1 blog Shinyanga
Endapo una Habari,Picha,Video,Tangazo au Tatizo Lolote wasiliana nasi kwa namba +255 688 405 951