MAAFA MAKUBWA YATOKEA KAHAMA,JESHI LA POLISI HALINA TAARIFA

Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga Justus Kamugisha

Mkuu wa wilaya ya Kahama Benson Mpesya

Watu wanane ambao ni wachimbaji wadogo wa dhahabu wanahofiwa kufa kwa kufukiwa na udongo katika machimbo ya Kalole kata ya Lunguya Wilayani Kahama Mkoani Shinyanga na mwingine kupigwa risasi ya tumbo na askari polisi katika ugomvi wa kugombea jiwe la dhahabu.

Wakati matukio hayo yakitokea baadhi ya wachimbaji wamedai hali hiyo inatokana na jeshi la polisi kutokuwa na ushirikiano na jamii ya maeneo hayo na kumtaka mkuu wa jeshi hilo nchini kufanya mabadiliko ya haraka wilayani humo ili kunusuru dhana ya polisi jamii.

Tukio la kwanza la wachimbaji hao kufukiwa na kifusi linadaiwa kutokea desemba 15 mwaka jana majira ya jioni wakati wachimbaji hao walipokuwa ndani ya moja ya mashimo yaliyopo katika eneo hilo la mgodi unaomilikiwa na Maulid wakati wakigombea kuchimba mchanga wa dhahabu.

Baadhi ya wachimbaji wakiwemo Abduh Juma,John Mwita ambao ni wakazi wa Tinde  Shinyanga na Nzega mkoani Tabora walisema  kuwa baada ya wenzao kufukiwa walisitisha shughuli zote za mgodi huo na kuanza kuwafukua wenzao kwa saa saba na kufanikiwa kuokoa wachimbaji wawili waliowaopoa wakiwa hai kabla ya wachimbaji waliookolewa kutoroshwa na polisi wasitoboe siri kwa wanahabari na mpaka sasa hawajulikani walipo.

’’Baadaye na sisi tulikata tamaa na kuamua kuwaacha wenzetu wakiwa shimoni maana kila tuliyekuwa tukimfuata alitupuuza kana kwamba hakuna tukio lililotokea eneo lile’’,alisema Juma kwa masikitiko.

Hata hivyo siku iliyofuata kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hiyo ikiongozwa na mwenyekiti wake Benson Mpesya ilifika eneo hilo na kuahidi kuleta vifaa vya uokoaji lakini haikufanya hivyo.

Hata hivyo mkuu wa wilaya alipotafutwa hakukiri wala kukanusha kuwepo kwa tukio hilo na badala yake alidai kuwa yuko jijini Mbeya msibani na kuahidi kuzungumzia tukio hilo baada ya msiba huo kumalizika.

Kufuatia hali hiyo,uongozi wa mgodi huo kwa kushirikiana na polisi umeamua kujenga kaburi   juu ya eneo waliofukiwa wachimbaji hao ili kuzuia wachimbaji wengine kufika eneo hilo.

Mwenyekiti wa wachimbaji wadogo mkoa wa shinyanga(SHIREMA) Nicodemus Majabi amekiri kutokea kwa tukio hilo ila akakanusha idadi hiyo akidai waliofukiwa ni watatu na wawili waliokolewa huku mmoja aliyemtaja kwa jina moja la Mussa ikishindikana kumuokoa kutokana na udongo wa eneo hilo kuwa tifutifu.

‘’Hili tukio lipo lakini waliofukiwa ni watatu na kati ya hao wawili waliokolewa na mmoja ndiyo bado yupo ardhini imeshindikana kumuokoa kutokana na udongo kuwa tifutifu’’alisema Majabi

Katika tukio la pili mchimbaji Kulwa Kashinje(32) ameuawa kwa kupigwa risasi na polisi wakati wakigombea jiwe linalodhaniwa kuwa na dhahabu.

Tukio hilo ambalo limetokea ndani ya mgodi huo unaodaiwa kufukia wachimbaji hao,limetokea Novemba 15,2014 mwezi mmoja kabla ya wachimbaji hao kufukiwa majira ya saa 12 jioni.

Imeelezwa baada ya polisi huyo aliyefahamika kwa jina la utani la Cheupe kumpiga risasi mchimbaji huyo alihamishwa kutoka katika kituo cha polisi wilaya ya Kahama na  haijajulikana alikohamishiwa.

Kamanda wa polisi Mkoa wa Shinyanga Justus Kamugisha alidai hana taarifa za matukio hayo na kuahidi kufuatilia ili kujua ukweli halisi wa matukio hayo mawili.
Na Valence Robert-Kahama

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post