Baadhi ya wakazi wa manispaa ya Shinyanga wamelalamikia kitendo cha kutokufunguliwa
kwa ofisi ya mbunge wao, Stephen Masele hali ambayo wamedai inachangia kwa
kiasi kikubwa wakose sehemu ya kuelezea kero mbalimbali zinazowakabili katika
maeneo yao.
Mbali
ya kutokufunguliwa kwa ofisi pia wakazi hao wamelalamikia kitendo cha simu ya
mbunge huyo kutopatikana muda wote pale anapotafutwa kwa njia ya simu na kwamba
namba yake aliyokuwa ameitoa kwa wapiga kura mara baada ya kuchaguliwa ya 0767 286
000 hivi sasa haipo hewani kwa kipindi kirefu.
Wakizungumza
na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki iliyopita wakazi hao walisema Jimbo la
Shinyanga hivi sasa linaonekana kama halina mwakilishi kutokana na wakazi wake
kukosa mtu wa kumfikishia matatizo yao baada ya mbunge wao kuteuliwa kushika
wadhifa wa Naibu waziri wa nishati na madini.
Walisema
pamoja na nafasi aliyopewa mbunge wao kuwa na mchango mkubwa katika maendeleo
ya jimbo lao lakini hata hivyo ingekuwa ni vizuri akaweka utaratibu mzuri
utakaowawezesha wao kuwa na mawasiliano naye ya mara kwa mara kwa kuweka mtu
mahsusi wa kukaa ofisi katika nyakati zote za muda wa kazi wa kiofisi.
Mmoja
wa wakazi hao, Madeleke Stephen mkazi wa eneo la Chibe alisema wapiga kura wa
jimbo la Shinyanga wanasikitishwa na kitendo cha kutofunguliwa kwa ofisi ya
mbunge wao hali ambayo inasababisha wakose mtu wa kumweleza matatizo yao
kutokana na simu za mbunge huyo kutokuwa hewani muda wote.
“Ukweli
kitendo cha kutofunguliwa kwa ofisi ya mbunge kwa muda wote ni sawa na sisi
kukosa mwakilishi, maana hatuna sehemu ya kufikisha matatizo yetu, kibaya zaidi
hata njia rahisi ya mawasiliano ya simu imeshindikana, maana ni rahisi zaidi kupata
simu ya Rais Kikwete (Jakaya) kulikoni ya mbunge Masele,” alieleza Stephen.
Kwa
upande wake mmoja wa makada wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mjini Shinyanga ambaye
hata hivyo hakupenda kutajwa gazetini alisema kitendo kinachofanywa na mbunge
wao kinaweza kusababisha madhara makubwa kwa chama chake wakati wa uchaguzi
mkuu wa Oktoba, 2015.
“Ni
kweli kuna malalamiko ya muda mrefu kuhusiana na suala la huyu mbunge wetu,
wananchi wengi wamekuwa wakihoji kitendo cha ofisi yake kutofunguliwa mara kwa
mara, awali alikuwa na msaidizi ambaye pia alikuwa ni katibu wa Jumuiya ya
wazazi wa CCM, lakini hivi sasa huyu ameacha kazi hiyo,”
“Baada
ya kuacha tunasikia ameajiriwa katibu mwingine, lakini ajabu bado wananchi
wanakwenda katika ofisi yake wanakuta imefungwa, sijui hizi shida za jimbo
zitapokelewaje? Ni haki wapiga kura kulalamika, tuna miezi michache kuelekea
uchaguzi mkuu, sasa huyu bwana ajisahihishe asije kukipa wakati mgumu chama
chetu wakati wa kampeni,” alieleza kada huyo.
Hata
hivyo kwa upande wake msaidizi wa sasa wa mbunge huyo, Mwajuma Rabia alikanusha
madai hayo na kueleza kwamba mara nyingi ofisi hiyo ipo wazi katika muda wote
wa saa za kazi na kuwaomba wananchi wasisite kupeleka matatizo yao.
Kuhusu
kutokupatikana kwa simu, Masele alikiri ni kweli muda mwingi amekuwa akifunga
simu zake kwa vile iwapo ataziacha hewani itakuwa vigumu kwake kutekeleza
majukumu mengine aliyonayo ya unaibu waziri wa Nishati na Madini na badala yake
atakuwa na kazi ya kupokea simu za wapiga kura muda wote.
“Ni
kweli kabisa simu zangu muda mwingi nazifunga, sipendi kuziacha wazi, maana
waandishi ninyi wenyewe mnaelewa kwamba nafasi niliyonayo hivi sasa
ninashughulikia watu wengi zaidi, hivyo iwapo nitaziacha hewani nitakosa muda
wa kushughulikia mambo mengine, muda wote itakuwa ni masuala ya jimbo tu,”
alieleza Masele.