TAARIFA KAMILI KUHUSU UVCCM KUFUNGA OFISI ZA CCM WILAYA NA DIWANI KUPIGWA SHINYANGA MJINI

Vijana wa UVCCM wakimsikiliza mwenyekiti wa CCM wilaya ya Shinyanga mjini Kanali mstaafu Tajiri Maulid aliyefika katika ofisi hizo baada ya kupata taarifa, aliwasihi vijana hao wafuate utaratibu kwa kuandika barua na kuwasilisha malalamiko yao-picha na Marco Maduhu-Malunde1 blog
Diwani wa kata ya Ndala Manispaa ya Shinyanga, Sungura George (mwenye shati la pundamilia)aliyepita jirani na ofisi hizo za CCM akitokea ofisi za afya za manispaa ya Shinyanga akisukumwa na Vijana wa CCM wilaya ya Shinyanga mjini  baada ya kuvamiwa ghafla na vijana hao na kushambuliwa kwa kuchapwa makofi-picha na Marco Maduhu-Malunde1 blog



Mzimu wa Uchaguzi wa serikali za mitaa Tanzania umeendelea kuitesa CCM mkoani Shinyanga ambapo katika hali isiyokuwa ya kawaida baadhi ya vijana wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Shinyanga mjini wamefunga kwa saa kadhaa ofisi ya CCM wilayani humo wakishinikiza kuondolewa kazini kwa katibu wa wilaya hiyo Charles Sangula.

Tukio hilo limetokea jana saa tatu asubuhi katika ofisi za CCm wilaya ya Shinyanga mjini ambapo mbali ya kumkataa katibu huyo pia vijana hao zaidi ya 20 waliwakataa katibu mwenezi wa wilaya, Charles Shigino na mchumi wa wilaya, Ahmed Mapalala wakidai kuwa sio waadilifu na wanawadharau UVCCM.

Inaelezwa kuwa viongozi hao wanawatuhumiwa kuchangia kushindwa kwa wagombea wa CCM katika uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika kote Desemba 14,mwaka huu.

Vijana hao wamemuomba mwenyekiti wa CCM Taifa, Jakaya Kikwete na katibu mkuu, Abdulrahman Kinana wachukue hatua mara moja za kuwaondoa madarakani watendaji hao wanaodaiwa kufanya mikakati michafu ya kutaka kukiuza chama hicho na kwamba kitendo chao kinaweza kuleta madhara makubwa katika uchaguzi mkuu wa mwezi Oktoba mwaka huu.

Wakizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za CCM wilaya ya Shinyanga mjini vijana hao walidai hatua yao ya kuwakataa viongozi hao wakuu wa wilaya inatokana na kupata ushahidi kwamba kushindwa kwa CCM katika mitaa mingi manispaa ya Shinyanga walihusika kwa njia moja ama nyingine.

Walisema hata hivyo viongozi hao wamekuwa hawatoi ushirikiano kwao (UVCCM) na mara nyingi huwadharau na kutowathamini pamoja na kwamba mchango wao ndani ya chama ni mkubwa lakini hawapewi ushirikiano wa kutosha kutoka kwa viongozi hao hali iliyochangia CCM kupoteza mitaa mingi katika manispaa ya Shinyanga.

Mmoja wa vijana hao Samwel Jackson mkazi wa kata ya Masekelo manispaa ya Shinyanga alisema waliamua kufunga ofisi hizo kwa lengo la kuwazuia katibu wa CCM wilaya, mwenezi wake na mchumi wa wilaya wasiingie ofisini baada ya kuchoshwa na vitendo vyao vinavyoashiria usaliti ndani ya chama.

“Tumechukua hatua hii kwa nia nzuri tu, vijana tumefanya uchunguzi wetu na kubaini kuwa wenzetu hawa walihusika kwa njia moja ama nyingine kuchangia kushindwa kwa wagombea wa CCM katika uchaguzi wa serikali za mitaa manispaa ya Shinyanga ambapo wagombea wengi wa CHADEMA walishinda katika mitaa mingi”,alieleza Jackson.

“Katibu wa CCM wa wilaya,mara kwa mara amekuwa akitudharau na wakati mwingine huwashusha vijana katika gari lake kwa madai ya kutowatambua hali ambayo imekuwa ikituvunja moyo, tuna mapenzi makubwa na CCM,hatuoni sababu ya kujitoa badala yake viongozi hawa  ndiyo waondolewe”,aliongeza Jackson.

 Hata hivyo kwa wakizungumza na waandishi wa habari kwa  nyakati tofauti watuhumiwa hao, ambao wamedaiwa kuwadharau vijana hao wa CCM,pamoja na kukihujumu chama, walikanusha tuhuma hizo na kudai hazina ukweli wowote, isipokuwa vijana hao wana lao jambo, huku wakihofia kuwa kuna mtu fulani kawapandikiza ili kukichafua Chama.


MWENYEKITI WA CCM AZUNGUMZA

Kwa upande wake mwenyekiti wa CCM wilaya ya Shinyanga mjini, Kanali mstaafu Tajiri Maulid aliyefika katika ofisi hizo baada ya kupata taarifa, aliwasihi vijana hao wafuate utaratibu kwa kuandika barua na kuwasilisha malalamiko yao ili yaweze kufanyiwa kazi ambapo pia aliwaomba waruhusu kufunguliwa kwa ofisi ili kazi ziweze kufanyika.

Kanali Maulid alisema haitokuwa rahisi kwa malalamiko yao kufanyiwa kazi iwapo ofisi hizo zitaendelea kufungwa na kwamba kulalamika kwa mdomo bila ya maandishi hakuna maana yoyote na kuwasihi waandike barua itakayojadiliwa katika vikao husika na kutolewa maamuzi.

“Andikeni barua na mueleze ni mambo gani mnayotaka yafanyiwe kazi, kumbukeni mambo ya chama hayatolewi maamuzi na mtu mmoja bali kinachofanyiwa kazi ni maamuzi ya vikao, tumepokea malalamiko yenu, fungueni mlango” ,alieleza Kanali Maulid.

Baada ya ushauri wa mwenyekiti huyo wa wilaya vijana hao walikubali kufungua ofisi hizo mnamo saa 3.50 asubuhi ambapo pia walikusanyana na kuanza hatua ya kuandika barua waliyoshauriwa kuiandika itakayoelezea malalamiko yao yote ikiwemo kupendekeza kuondolewa madarakani kwa viongozi wanaowakataa.
  
DIWANI WA CHADEMA APIGWA VIBAO

Katika sekeseke hilo diwani wa kata ya Ndala Manispaa ya Shinyanga, Sungura George aliyepita jirani na ofisi hizo za CCM akitokea ofisi za afya za manispaa ya Shinyanga alijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kuvamiwa ghafla na vijana hao na kumshambulia kwa kumchapa makofi matatu huku akitakiwa kupotea katika eneo hilo mara moja huku akinusurika kugongwa na gari. 

Kwa upande wake diwani wa CHADEMA kata ya Ndala, Sungura George alisema kufuatia kitendo cha kushambuliwa kwa kipigo na vijana hao wa CCM anakusudia kwenda kuwashtaki polisi ili sheria iweze kuchukua mkondo wake baada ya kuvamiwa na kupigwa bila sababu zozote alipokuwa akipita barabarani.

MGOGORO NDANI CCM WILAYA YA SHINYANGA MJINI
Tukio la vijana wa CCM linakuja siku chache tu baada ya  viongozi wa CCM kufikia hatua ya kutukanana matusi ya nguoni kutokana na kushindwa kufanya vizuri katika uchaguzi wa serikali za mitaa katika manispaa ya Shinyanga.

Desemba 15,2014 majira ya saa 5 na nusu asubuhi,katibu wa Siasa na uenezi wa CCM wilaya ya Shinyanga Mjini Charles Shigino na katibu wa umoja wa Vijana wilaya ya Shinyanga Mjini (UVCCM), Zawadi Husein Nyambo walitukanana matusi ya nguoni almanusura wachapane makonde wakati Shigino akiingia katika ofisi za Chama, (mlangoni).

Inaelezwa kuwa wakati Shigino akiingia katika ofisi za chama ghafla alitokea katibu wa umoja wa vijana (UVCCM), Zawadi Hussein Nyambo, na kumzuia kuingia katika ofisi hizo,na kuanza kumrushia maneno machafu hali iliyosababisha mtafaruku mkubwa na kujaza umati wa watu.

Alisimulia mkasa  uliompata kwa waandishi wa habari Shigino alisema ugomvi huo ulikuja baada ya chama chake kufanya vibaya katika kata ya Ngokolo ambapo wapinzani wao Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema kupata ushindi katika  mitaa sita huku CCM, wakiambulia mtaa mmoja pekee huku mwanaCCM huyo akimtuhumu kuwa yeye ndiye kasababisha matokeo hayo kuwa mabovu.

Katibu huyo wa umoja wa Vijana wilaya ya Shinyanga Mjini (UVCCM), Zawadi Hussein Nyambo alisema alimzuia katibu mwenezi huyo kuingia katika ofisi za chama hicho kwa madai kuwa yeye ni msaliti wa chama na amekuwa akitoa siri na kuzipeleka kwa wapinzani.


Katika uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika Desemba 14,2014, kati ya mitaa 55 katika wilaya ya Shinyanga Mjini, CCM, walipata ushindi katika mitaa 26 huku (CHADEMA) wakipata mitaa 29, na katika kata ya Ngokolo yenye mitaa 7, CHADEMA walipata mitaa 6 huku CCM wakiambulia mtaa mmoja pekee, matokeo ambayo yamesababisha ugomvi ndani ya (CCM) wakisaka mchawi wao.

Na Kadama Malunde-Shinyanga  

Bonyeza hapa Tukupe habari zote mara moja zikitoka  
Endapo una Habari,Picha,Video,Tangazo au Tatizo Lolote wasiliana nasi kwa namba  +255 688 405 951

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post