Waandamanaji wakichoma matairi ya magari
Polisi katika Jamuhuri ya
kidemokrasi ya Congo, wamefyatua risasi hewani ili kuwatawanya
waandamanaji waliokuwa wamekusanyika katika mji mkuu Kinshasa kupinga
sheria mpya ya uchaguzi.
Serikali inasema kuwa watu wanne
walifariki katika vurugu za Jumatatu ingawa upinzani unasema idadi huo
huenda ikawa juu kuliko iliyonakiliwa.
Wanafunzi wameweka vizuizi
barabarani na pia wameshuhudiwa wakichoma magurudumu, katika barabara
zinazoelekea katika chuo kikuu mjini humo.
Wanatuhumu wanasiasa
wanaomuunga mkono Rais Joseph Kabila ambaye muhula wake wa pili
unatarajiwa kumalizika mwaka ujao kwa kujaribu kujiongeza muda mamlakani
kwa kuidhinisha mipango ya kufanyika sensa ambayo itachelewesha
uchaguzi kwa miaka mingi.
Vurugu hizi zinashuhudiwa huku baraza la
Senate likidadisi mswada ambao huenda ukasababisha Rais Kabila
kuongezwa muda mamlakani.
Vijana walioandamana kwa vurugu, waliteketeza magurudumu ya magari, kupora maduka na kurusha mawe.
Wanafunzi waliambia BBC kuwa polisi walivamia chuo chao baada ya wao kuanza kuandamana.
Walisema polisi waliingia katika vyumba vyao na kuwafyatulia gesi ya kutoa machozi.
Viongozi
wa upinzani walitoa wito kwa waandamanaji kwenda barabarani kupinga
mipango ya serikali kumuongeza muda zaidi mamlakani Rais Joseph Kabila
huku wakiutaja mpango huo kuwa mapinduzi ya kikatiba.
Mswada huo unapendekeza kufanyika sensa kote nchini ambayo itachukua kipindi cha miaka mitatu.
Rais Kabila amekuwa mamlakani tangu mwaka 2001. Muhula wake wa pili unakamilika mwaka 2016 kikatiba.
via>>BBC
via>>BBC
Endapo una Habari,Picha,Video,Tangazo au Tatizo Lolote wasiliana nasi kwa namba +255 688 405 951