WALINZI WAVUNJA OFISI ZA KAMPUNI YA JAMBO GINNERY SHINYANGA,WAIBA PESA NA KUTOWEKA NA BUNDUKI 2

 
Jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga linawasaka walinzi wawili wa kampuni ya Prosper Security Guard kwa kosa na kuvunja ofisi ya Jambo Oil Mill and Ginnery Limited kisha kuiba fedha shilingi milioni 1,070,000/= na kutoweka na bunduki mbili aina ya Shortgun na risasi 7.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari,kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga Justus Kamugisha(pichani) alisema tukio hilo limetokea Januari 9,2015 saa moja asubuhi katika eneo la mtaa wa Ibadakuli kata ya Ibadakuli manispaa ya Shinyanga.

Kamanda huyo alisema siku hiyo mkurugenzi wa Jambo Ginnery Mohamed Hawadhi(48) aligundua ofisi ya kampuni imevunjwa na kuibwa fedha taslim shilingi 1,070,000/= zilizokuwa ndani ya kasiki la chuma mali ya kampuni hiyo.

Kamanda Kamugisha aliongeza kuwa katika tukio hilo walinzi wawili wa kampuni ya ulinzi ya Prosper Security Guard waliokuwa wakilinda ofisi hiyo walitoweka na bunduki mbili aina ya Shortgun zenye namba F658126 na R65967 pamoja na risasi 7.

Aliwataja walinzi hao kuwa ni William Ubogo na Eliamani Simoni ambao bado wanatafutwa  na jeshi la polisi ili wakikamatwa hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao.

Hata hivyo Kamanda Kamugisha alisema baada ya jeshi la polisi kupata taarifa juu ya uhalifu huo lilifanya msako mkali na Januari 10,2015 saa 6:00 mchana lilifanikiwa kupata silaha zote mbili na risasi 7 zikiwa zimetelekezwa katika maficho karibu na kiwanda hicho.
Na Kadama Malunde-Shinyanga

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post