WANANCHI WAUA KWA MAWE NA MARUNGU KISHA KUCHOMA MOTO JAMBAZI LENYE SMG

Kamanda wa polisi mkoa wa Geita Joseph Konyo

Wananchi katika kisiwa cha Izumacheli Kata ya Nkome Wilayani Geita mkoani Geita, wamefanikiwa kumuua mtuhumiwa wa ujambazi akiwa na SMG yenye risasi 28, kwa kumshambulia na mawe pamoja na marungu kisha mwili wake kuuteketeza kwa moto hadi ukawa majivu.

Mtuhumiwa huyo,alikamatwa akijiandaa kufanya uharifu kwenye kisiwa hicho akiwa  na silaha hiyo ya aina ya SMG na Risasi 28 iliyofutwa namba.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Joseph Konyo, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kumtaja aliyeuawa kuwa ni Mawazo Nagabona(43)mkazi wa kisiwa cha Ikuza Wilayani Mreba Mkoani Kagera.

Alisema tukio hilo lilitokeajana saa 11 alfajiri baada ya wananchi wa kisiwa hicho kupata taarifa kwamba mtuhumiwa na wenzake ambao hawajakamatwa wamepanga kufanya uharifu kwenye kisiwa hicho kwa kuwapora wafanyabiashara na wavuvi wa kisiwa hicho mali zao.

Hata hivyo kamanda Konyo alifafanua kuwa,wananchi hao walifanikisha kubaini hilo kutokana na mafunzo ya polisi jamii  waliyoyapata na kuwajengea uwezo wa kutambua waharifu na namna ya kupashana habari namna ya kuchukuwa hatua kwenye matukio ya dharula kama hilo.

“Baada ya kupata taarifa za majambazi hao wananchi hao  walianza kumzingira na baadaye jambazi huyo aliwapeleka ilipo Bunduki yake aliyokuwa ameihifadhi kwenye mtumbwi na ndipo walipochukuwa jukumu la kumshambulia kwa mawe na malungu kisha kumchoma moto  kabla ya polisi kufika na kumkuta akiwa ameteketea kwa moto na kubaki majivu’’ alisema Kamanda Konyo.

Aliongeza kuwa,iwapo jeshi la polisi lingekuwa na boti yake lingewahi eneo la tukio kabla ya mtuhumiwa huyo kuuawa na lilichelewa kutokana na mazingira ya kufika eneo hilo kuwa magumu na hatarishi na kuwataka wananchi kuacha kujichukulia sheria mkononi  wanapokuwa wamefanikiwa kuwadhibiti waharifu na badala yake wawafikishe kwenye vyombo vya dola.

‘’Haki ya kuishi ni haki ya kikatiba na inapotokea wananchi wamemuua mtuhumiwa wanakuwa wamepunguza tatizo kidogo maana wanafanya kazi ya kuwapata wenzake kuwa ngumu lakini kama mtuhumiwa akiwepo atawataja anaoshilikiana nao na inakuwa kazi rahisi kukamata mtandao wake’’alisema Konyo.

Hili ni tukio la pili kutokea katika kipindi cha miezi 6 iliyopita ambapo Juni 24 mwaka jana watuhumiwa wa ujambazi walizua taharuki mjini Geita baada ya kuvamia  mchana kweupe kwenye duka la mfanyabiashara wa bia la Blue Coast Investment, linalomilikiwa na Ignas Athanas na kupora fedha kisha kuondoka baada ya kupiga risasi moja hewani, kuwatisha watu.
Baada ya hapo, walivamia katika duka la wakala wa kampuni za simu, ambapo yalipora fedha na kumuuwa kwa risasi mmiliki wa duka hilo Gosbert Kulwa (59), maarufu kwa jina la Warwa. Pia walimpora bastola na baadaye majambazi hao waliuawa na wanafunzi wa shule ya Sekondari Nyang’hwale Mkoani Geita wakati wakijaribu kutoroka wakitumia pikipiki aina ya Sun LG yenye namba T460 CVQ, yaliyoondoka nayo  kwa kasi huku yakinusurika kugongwa na basi la Sabuni lililokuwa likitokea Mwanza kwenda Mganza, wilayani Chato.

Wakati wa tukio hilo, shughuli zilisimama kwa muda katika mji wa Geita,  huku watu wakikimbia ovyo kuokoa maisha yao kabla ya polisi kufika na kuanza kuyafuatilia kabla ya kukuta wanafunzi hao wamekwishayaua na kufanikiwa kuokoa bastora yaliyopora pamoja na SMG waliyokuwa wakiitumia.
Na Victor Robert-Malunde1 blog Geita

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post