Siku chache baada ya
serikali kupiga marufuku upigaji ramli nchini kwa madai kuwa inachangia
kwa asilimia kubwa mauaji na ukatwaji wa viungo vya watu wenye
albinism, baadhi ya waganga wanaojishughulisha na vitendo hivyo
wamepinga agizo hilo huku jukwaa la tiba asili likipongeza hatua hiyo ya
serikali.
Kufuatia agizo hilo la serikali ITV ilitaka kufahamu wahusika na
wadau mbalimbali wa tiba za asili wamelipokeaje agizo hilo ambapo
imefanikiwa kuzungumza na mzee Shabani Rajabu ambaye pia ni mwenyekiti
wa chama cha waganga na wakunga wa jadi nchini na anajishughulisha na
upigaji ramli ambapo amesema serikali inatakiwa kuwa makini katika
kuendesha zoezi hilo kwani yenyewe inahusika kutoa vibali na kuongeza
kuwa siyo ramli zote ni chonganishi.
Kwa upande wa jukwaa la tiba asili Tanzania
mbali na kupongeza agizo hilo la serikali wameitaka kwanza kutoa elimu
kwa njia mbalimbali kwa wananchi kwani asilimia kubwa wanahusisha ramli
kama sehemu ya matibabu au kugundua magonjwa lakini pia baadhi ya
watawala wamekuwa wakitumia ramli hizo wakidhani zitaweza kuweka mambo
yao sawa katika nyadhifa zao huku wakiitaka serikali kuwa makini katika
kutoa vibali kwa waganga hao.
Agizo la kupiga marufuku upigaji ramli nchini lilitolewa jijini Dar es salaam
hivi karibuni na waziri wa mambo ya ndani ya nchi Mh. Mathias Chikawe
ambaye alisema timu ya watu sita wakiwemo askari na watu wenye albinisim
itaendesha operesheni maalum ya kusaka watu hao kama njia mojawapo ya
kukabiliana na tatizo la mauaji ya albino hapa nchini ambayo alikiri
kuongezeka mwishoni mwa mwaka jana.
Endapo una Habari,Picha,Video,Tangazo au Tatizo Lolote wasiliana nasi kwa namba +255 688 405 951