Mahakama ya wilaya ya Chato mkoani Geita imewahukumu kifungo cha
miaka mitano jela kila mmoja,Joseph Christopher(25) mkazi wa kijiji cha
Nkome na Bahati Juma(28) mkazi wa kijiji cha Katoro wilayani Chato baada
ya kupatikana na hatia ya kujiita maofisa wa jeshi la polisi kwa lengo
la kufanya utapeli.
Katika kesi hiyo washitakiwa wamedaiwa kufanya utapeli katika
kijiji cha Buseresere na kufanikiwa kupora simu mbili aina ya TECNO na
NOKIA pamoja na kujipatia shilingi 11,000 kinyume cha sheria.
Akiielezea mahakama hiyo,Mkuu wa polisi wilaya ya Chato (OCD), Bw. Alex Mukama, kwa niaba ya mwendesha mashitaka wa polisi amesema
washitakiwa hao walitenda kosa hilo kwa lengo la kujipatia fedha na simu
baada ya kujitambulisha kuwa wao ni maofisa wa jeshi la polisi na
kwamba walikuwa wametumwa kijijini hapo kufanya upelelezi kwa wahalifu.
Aidha baada ya kutumia ulaghai huo walilazimika kuwaomba vijana
wawili simu zao pamoja na fedha kiasi cha shilingi 11,000 kisha
kutokomea nazo huku vijana hao wasijue la kufanya,na baada ya muda
kitambo walifanikiwa kumwona mmoja wa matapeli hao akiwa kwenye stendi
ya mabasi na ndipo walipiga yowe kwa lengo la kuomba msaada kwa
wasamaria wema kisha kumkamata na kumfikisha kwenye kituo cha polisi
Buseresere.