ANGALIA PICHA- KATIBU WA CUF SHINYANGA AVURUGWA NA WANAWAKE,ATAKA KUPIGA WAANDISHI WA HABARI

Wakazi wa Shinyanga wakiwa nje ya ofisi za CUF mjini Shinyanga wakishinikiza kupewa pesa zao baada ya kuzungushwa kila siku na kudai kuwa Chama hicho kinataka kuwatapeli pesa zao,ambapo kufuatia kuvurugwa na watu hao Katibu wa CUF wilaya ya Shinyanga mjini Said Sizya alihamishia hasira zake kwa waandishi wa habari waliofika kwenye ofisi hizo kuchukua matukio yaliyokuwa yanaendelea
Nje ya ofisi za Chama Cha Wananchi CUF wilaya ya Shinyanga mjini mkoani Shinyanga ambapo kundi la akinamama zaidi ya 50 wengine wakisindikizwa na waume zao wamefika katika ofisi hizo kudai mikopo yao waliyoahidiwa na viongozi wa Chama hicho baada ya kutoa shilingi 12,500/= na shilingi 500/-=kwa ajili ya kadi ya chama hicho jumla shilingi 13,000/= ili wapewe shilingi 300,000/= bila riba yoyote lakini tangu mwezi wa Januari mwaka huu hawajapatiwa

Akina mama wakiwa eneo nje ya ofisi wakishuhudia katibu wa CUF wilaya ya Shinyanga mjini akiwarushia maneno machafu waandishi wa habari waliofika eneo hilo kutimiza wajibu wao,ambapo pia akiwa na viongozi wenzake waliwatishia kuwapiga na kuwavunjia kamera zao na kuwataka waondoke eneo hilo kwani malalamiko ya akina mama hayo hayawahusu waandishi wa habari

Wa kwanza kushoto ni katibu wa CUF wilaya ya Shinyanga mjini Said Sizya akitukana waandishi wa habari( hawako pichani)
Akina baba hawakuwa nyuma nao walijisogeza kushuhudia kilichokuwa kinajiri kwenye ofisi hizo za CUF mjini Shinyanga

Wananchi wakimshangaa katibu huyo kugombana na waandishi wa habari wakati wamekuja kusikiliza malalamiko

Katibu wa CUF wilaya ya Shinyanga mjini Said Sizya akiendelea kukabiliana na waandishi wa habari walioonesha kutotishika pamoja na kuwepo kwa vitisho vya hapa na pale kutoka kwa viongozi wa CUF

Aliyenyosha mkono juu(nguo nyeupe)  ni mmoja wa viongozi wa CUF ambaye ndiye alikuwa anaandikisha majina ya akinamama sambamba na kuwauzia kadi za CUF kwa shilingi 500 ili wachukue mkopo,naye bila aibu akitukana waandishi wa habari

+++++++++++++++++++++++++
Ofisi za Chama cha Wananchi CUF wilaya ya Shinyanga Mjini mkoani Shinyanga zimegeuka uwanja wa matusi baada ya baadhi ya viongozi wake wakiongozwa na katibu wa wilaya hiyo Said Sizya kutaka kuwapiga na kuwavunjia vifaa vyao vya kazi waandishi wa habari waliofika katika ofisi za chama hicho kuchukua matukio baada ya kupewa taarifa kuwa kundi la wanawake zaidi ya 50  limeandamana katika ofisi hizo wakidai kudhulumiwa pesa walizotoa kwa ajili ya kupatiwa mkopo.


Waandishi wa habari  waliojikuta wanafanya kazi zao katika mazingira magumu ni Suzy Butondo wa gazeti la Mwananchi na The Citizen,Kadama Malunde wa gazeti la Mtanzania na Kahama FM ambaye pia ni Bloga Maarufu kupitia www.malunde1.blogspot.com na Emmanuel Mpanda mwakilishi wa Zanzibar Television.

Waandishi hao wa habari walifika katika ofisi za chama hicho jana majira ya saa 10 jioni baada ya kupewa taarifa kuwa wanawake zaidi ya 50 kutoka maeneo mbalimbali ya manispaa ya Shinyanga wameandamana wakidai kudhulumiwa pesa walizotoa kwa ajili ya kupewa mkopo wa fedha na chama hicho.

Walioshuhudia tukio hilo walieleza kuwa wakati waandishi hao wa habari wanafanya mahojiano na wanawake hao nje ya ofisi za chama hicho kujua nini hasa kimewafikisha hapo,ghafla walijitokeza viongozi wa CUF wakiongozwa na katibu wa chama hicho Said Sizya wakiwa wamehamaki kutokana na kile kilichoelezwa kuwa wamevurugwa na akina mama hao.

Walisema viongozi hao wakiongozwa na Sizya waliwataka waandishi hao wa habari waondoke haraka katika eneo hilo kwa madai kuwa hawatakiwi kufanya kazi za uandishi katika eneo  bila kuwataarifu viongozi wa chama hicho na kwamba walitakiwa wawaulize kwanza wao kwanini akina mama hao wapo mahali hapo badala ya kuanza kuzungumza na wananchi moja kwa moja.


“Ondokeni haraka sana hapa,mmekuja kufanya nini,nani kawaita,mnataka kuleta vurugu kwa watu wetu,tutawapiga na tutavunja kamera zenu sasa hivi,hatutaki mpige picha mahali hapa,haya mambo hayawahusu”,walisikika wakisema viongozi hao wa CUF,walieleza mashuhuda hao.


“Mmekuja hapa bila taarifa,hamjafuata utaratibu mlitakiwa muongee na sisi viongozi kwanza ,Ondokeni sitaki kuwaona,hapa ni mahali pangu,sitaki muongee na watu wangu,sitaki kuzungumza na nyinyi,sitaki hata muingie ofisini kwangu,nendeni mkatangaze kwenye vyombo vyenu”,alisema Katibu wa CUF huku akiwasukuma waandishi hao wa habari.

Pamoja vitisho hivyo kutoka kwa viongozi hao wa CUF wakiongozwa na katibu wao,waandishi wa habari hawakusaliti maadili ya kazi yao katika kuihabarisha jamii hivyo kulazimika kufanya kazi katika mazingira magumu ya vitisho vya hapa na pale ikiwemo kukatazwa kupiga picha na kutishiwa kuvunjiwa kamera zao.

Wakizungumza na waandishi wa habari nje ya ofisi hizo akina mama hao ambao walikuwa na kadi za CUF ikiashiria kuwa ni wanachama wa chama hicho ,waliuomba uongozi wa Chama hicho kuwapatia mkopo wao kama walivyowaahidi kuwasaidia kuinua uchumi wao badala ya kutoa ahadi hewa na kuwapa matumani ya kupata pesa hizo kila siku.

“ Sisi mwezi Desemba 2014 tulitangaziwa na CUF kuwa kuna mikopo inayotolewa kwa akina mama bila riba ya aina yoyote,kiingilio shilingi 12,500/= na kadi ya CUF unayopaswa kuilipia shilingi 500/= jumla shilingi 13,000/= baada ya hapo wakatuahidi watatupatia mkopo wa shilingi milioni 1.5 kwa kila kikundi cha watu watano tarehe 28,Januari 2015 lakini mpaka sasa wanatuzungusha tu”,alisema Annastazia Yasin.

“Kilichotuleta hapa, tunalalamikia pesa zetu tarehe 27 Desemba waliahidi kutupatia pesa Januari 28,2015 lakini hadi leo bila bila, kila siku tunakuja kufuatilia pesa zetu ,tunachohitaji sisi ni mkopo wetu kwani wengine tumekopa pesa kwa watu ili kujiunga kupata mkopo kwa ajili ya shughuli mbalimbali ikiwemo ujasiriamali”,Justina Simon.

Kwa upande wake mmoja wa wakazi wa Shinyanga Maganga Ng’wagi aliyekuwa ameambatana na mke wake Joyce Musa katika ofisi hizo aliwaomba viongozi wa CUF kutekeleza ahadi zao kwa wakati na kama walivyoahidi kwa mara nyingine kutoa mikopo hiyo siku ya Jumatano wiki ijayo.

“Ndugu waandishi ,wakati mwingine sisi tuliooa tunapata wasiwasi kila siku mke wako anaaga kufuata mkopo lakini hauuoni,nini maana yake sasa,hawa ndugu zetu wajitahidi tu kutekeleza wanayoyasema,sisi hatuna ugomvi nao,kwani wanataka kutusaidia”,alieleza Ng’wagi.

Hata hivyo baadhi ya wakazi wa Shinyanga walioshuhudia tukio hilo walieleza kusikitishwa na kitendo cha katibu huyo wa CUF kugeuka mbogo kwa waandishi wa habari waliofika eneo hilo kutimiza wajibu wao huku wakiongeza kuwa pengine kuna jambo ka siri katika ofisi hiyo.
  Na Mwandishi wetu Shinyanga mjini

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post