WATANZANIA WENGI WANAPATA MAGONJWA YASIYOAMBUKIZWA KWA KASI YA AJABU

Mganga mkuu wa mkoa wa Shinyanga Dkt Ntuli Kapologwe (picha kutoka maktaba yetu)

 Imeelezwa kuwa watanzania wengi wanapata  magonjwa  yasiyoambukizwa  ikiwemo kisukari,presha,saratani na moyo kutokana na  kutozingatia ulaji wa vyakula pamoja kuendekeza uvutaji wa sigara na kunywa pombe  kupita kiasi  hali ambayo imefanya idadi  ya wagonjwa  kuongezeka kila siku na kufikia asilimia 67.

 
Hayo yamesemwa juzi na Dkt Digna  Narciss  ambaye ni bingwa wa magonjwa yasiyoambukizwa kutoka  katika hospitali ya Amana  ya jijini Dar es salaam wakati wa zoezi  la upimaji  magonjwa yasiyoambukizwa kwa wakazi wa Shinyanga lililofanyika katika hospitali ya mkoa huo.

Dkt  Narciss  alisema magonjwa  kama kansa,presha,kisukari na moyo  yanasababishwa na tabia ya kutozingatia ulaji wa vyakula vya mboga za majani,uvutaji  wa sigara na  unywaji wa pombe kupita kiasi pamoja na uzito uliokithiri.


Alisema kwa mujibu wa Shirika la afya Duniani( WHO) utafiti  unaonesha kuwa mwaka 2011 watu milioni 300 duniani waligundulika kuwa na ugonjwa  wa kisukari na kufikia mwaka 2030  kuna uwezekano wa kufikia  watu milioni 520.

Aliongeza mwaka 2011 watu waliobainika kuwa ugonjwa wa  presha  duniani ni  milioni 600 kwa  mwaka 2011 na maksio ya kufikia  mwaka 2025 ni watu bilioni  moja na nusu.

Naye mganga mkuu wa mkoa  wa Shinyanga  Dkt Ntuli  Kapologwe alisema katika kipindi cha mwezi Januari hadi Desemba mwaka 2014 asilimia 12 wa wakazi wa Shinyanga walibainika kuwa na  magonjwa yasiyoambukizwa ikilinganishwa na mwaka 2013 ambapo ilikuwa ni asilimia 5.


Dkt Kapologwe alitumia fursa hiyo kuwataka wananchi kuwa na  utaratibu wa kupanga lishe, kupunguza unywaji wa pombe,kutotumia zaidi vyombo vya usafiri na kufanya mazoezi.

Katika hatua nyingine aliwataka wananchi kujitokeza kupeleka watoto wao katika vituo vya afya kwani idadi ya watoto imekuwa ni ndogo kutokana na imani iliyojengeka kuwa  watoto wadogo  hawana magonjwa hayo lakini wapo baadhi ya watoto wenye kupatwa, ni vyema nao wakapimwa.

Na Kadama Malunde-Shinyanga

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post