HII NDIYO SABABU YA MWANAHARAKATI NA MSHIRIKA WA LOWASSA KUSHIKILIWA NA POLISI

 
JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam kwa kushirikiana na Idara ya Uhamiaji nchini, wanafanya uchunguzi kuhusu tuhuma zinazomkabili mwanaharakati na mshirika wa aliyekuwa mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Edward Lowassa, Bashir Awale anayetuhumiwa kuwa Mkenya.

Awale aliyekuwa mwanaharakati wa Lowassa katika mchakato wa kuelekea Ikulu, alikamatwa Novemba 9, mwaka huu, akituhumiwa kwa utata wa uraia wake na jinsi alivyokuwa akijihusisha na siasa nchini. Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova aliyasema hayo jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.

Kova alisema baada ya kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo, alipekuliwa nyumbani kwake maeneo ya Mikocheni, na alikutwa na cheti cha kuzaliwa chenye namba D 063711 kwa jina la Bashir Ally.

Alisema cheti hicho kinaonesha kuwa alizaliwa Julai 11, 1969 katika Hospitali ya Serikali mkoani Dodoma. Aidha, alisema pia mtuhumiwa alikutwa na hati ya kusafiria ya Kenya yenye namba C 000529 ambayo ilionesha kuwa alizaliwa Nairobi tarehe hiyo hiyo kwa jina la Bashir Awale.

“Kumbukumbu hizo zinakinzana na zinaleta utata, hivyo tunashirikiana na Idara ya Uhamiaji kumhoji mtuhumiwa kwani hilo ni kosa chini ya sheria za uhamiaji,’’ alisema Kova. Alifafanua kuwa zipo tuhuma zinazoonesha mtuhumiwa huyo akiwa raia wa Kenya, amekuwa akijihusisha na siasa za Tanzania hususan wakati wa Uchaguzi Mkuu mwaka huu.

“Kitendo hicho ni kinyume cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ambayo haimpi nafasi raia wa kigeni haki ya kuchagua, kuchaguliwa na kushiriki katika kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani,” alifafanua Kova.

Kova alisema kuwa mtuhumiwa huyo anachunguzwa na kwamba akibainika kuwa alijihusisha na siasa wakati sio raia, itakuwa ni kinyume cha Katiba, hivyo atachukuliwa hatua za kisheria. Alisema mtuhumiwa huyo hivi karibuni alipeleka maombi ya uraia katika Idara ya Uhamiaji, na hajakubaliwa.

Alisisitiza kuwa Watanzania wasiwe warahisi kukaribisha wageni kwani ni lazima kuwa na viwango kwa sababu ni hatari kwa usalama wa nchi. “Tuwe na kiasi kwani nchi za wenzetu hawana utaratibu wa kuruhusu wageni kuingia pasipo kuwa na kibali.

Tuige mfano huo ili tuendelee kuwa salama,’’ alisema Kova. Alisema hawamuonei mtuhumiwa huyo, bali sheria inawataka kufanya uchunguzi wa kina kuhusu tuhuma mbalimbali zilizoelekezwa kwake.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post