MCHUNGAJI WA KANISA NA MAMA MCHUNGAJI WATIWA MBARONI KWA KUMFUNGIA NDANI MIAKA 12 MTOTO WAO MWENYE ULEMAVU


POLISI mkoani Singida linamshikilia Mchungaji wa Kanisa la Pentekoste Itaja na mkewe kwa tuhuma za kumfungia ndani ya chumba mtoto wao mlemavu wa viungo kwa miaka 12 bila kutoka nje.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Thobias Sedoyeka aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni David Mtipa (59) ambaye ni Mchungaji wa Kanisa hilo na mkewe Mariam Philipo (45) wote wakazi wa kijiji cha Itaja katika tarafa ya Mgori wilayani Singida.


Kamanda Sedoyeka alisema tukio hilo liligundulika juzi katika kijiji hicho baada ya Polisi kupata taarifa za siri kutoka kwa wasamaria.

Akielezea tukio hilo, Kamanda Sedoyeka alisema watuhumiwa walimfungia ndani ya chumba mtoto huyo, Timotheo David (30) kwa muda wa miaka 12 huku huduma zote za kibinadamu, ikiwemo haja ndogo na kubwa pamoja na chakula zikifanyika humo ndani.


“Baada ya timu ya askari wa Upelelezi na Ofisa Ustawi wa Jamii kufika eneo hilo wakiwa na viongozi wa kijiji na kufanya mahojiano, watuhumiwa walikiri kumfungia chumbani mtoto wao huyo na kwamba ni mlemavu wa miguu na mikono, lakini pia ni mlemavu wa akili,” alisema Kamanda Sedoyeka na kuongeza:


“Wamesema mtoto wao alizaliwa mwaka 1984 akiwa mzima, lakini alipofika darasa la sita 2003 alianza kuugua ugonjwa usiojulikana ikiwa ni pamoja na kuanguka kisha kutoa povu mdomoni huku mwili wake ukibadilika rangi kuwa ya njano na kutibiwa bila mafanikio.”


Aidha, alisema mlemavu huyo alitibiwa maeneo mbalimbali bila mafanikio na ndipo wazazi hao walipoamua kumfungia ndani baada ya kuona wanafedheheshwa mbele ya jamii huku akila chakula, kujisaidia humo chumbani na kutoruhusiwa kutoka nje.


Kutokana na hali hiyo, majirani waliingiwa na hofu kwa kutomwona mtoto huyo kwa kipindi kirefu kiasi hicho hali iliyozua maswali mengi.

Wakati baadhi walijua huenda ameuawa, wengine walihusisha kitendo hicho na imani za kishirikina huku Mchungaji akidaiwa kuzidiwa maarifa na mkewe.


Alisema kitendo cha kumfungia mtoto huyo ndani kwa kipindi chote hicho, kumwacha akiwa uchi na kumlaza kwenye kitanda cha kamba kisichokuwa na godoro ilikuwa ni ukiukwaji wa misingi ya binadamu na si cha kiutu.


Alisema amepelekwa Hospitali ya Mkoa wa Singida kwa matibabu na uchunguzi zaidi wa afya yake wakati wazazi hao wakishikiliwa na kuhojiwa ili hatimaye wafikishwe mahakamani kwa ukatili uliovuka mipaka.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post