WAZIRI KITWANGA AIKANA ORODHA YA WAUZA UNGA,ADAI HANA MUDA WA KUSHUGHULIKA NAYO HIYO KITU INAYOITWA "ORODHA"




WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga amesema hana orodha ya majina ya watu wanaouza dawa za kulevya na hana muda wa kushughulika na hiyo inayoitwa orodha.

Badala yake, amesema chini ya uongozi wake ataweka mifumo itakayosaidia kudhibiti uingizaji wa dawa hizo nchini.

Akizungumza jana na waandishi wa habari Dar es Salaam baada ya kufanya kikao na maofisa wa ngazi ya juu wa Polisi, Kitwanga alisema wamekubaliana kuhakikisha dawa za kuleya zilizoko nchini zinakamatwa na kuteketezwa.


“Mimi hapa nilipo sina orodha ya wauza dawa za kulevya na wala Rais hajanipatia hiyo orodha na siamini kama Rais anayo...ila ninachowaambia ni kwamba tumekubaliana kuweka mifumo mizuri ya kuwakamata watu wote ambao watakutwa na dawa hizo,” alisema Kitwanga.


Alisema mifumo hiyo haitajali ukubwa na nafasi ya mtu kwenye jamii. “Maana mifumo hii tunayoiweka haijali vigogo wala sisimizi na nawahakikishia kwamba tumejipanga kumaliza tatizo hili la dawa za kuleya,” alisema.


Alisema katika kikao hicho wamekubaliana kuongeza nguvu kuhakikisha wanawakamata watu wote ambao wanahusika na biashara haramu ya kuingiza dawa za kulevya na kuzisambaza nchini.


Akizungumza kutokuwepo kwa polisi katika Bandari ya Dar es Salaam, alisema wanaendelea kufanya mazungumzo na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) kuona utaratibu mzuri wa kupeleka ulinzi kwenye eneo hilo ili kuweza kudhibiti utoroshaji wa vitu mbalimbali ambavyo vinatoka bila utaratibu.

Katika hatua nyingine, Kitwanga aliwataka polisi kuwashitaki watu kwa kesi walizo nazo na sio kuwabambika kesi watu wasio na hatia na kusababisha kufungwa kwa kesi zisizowahusu.




Via>>Mpekuzi blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post