AGPAHI Yafanya Bonanza la Michezo la Vijana – Uwanja wa Taifa wa Kahama Mji


Hapa ni katika uwanja wa taifa Mjini Kahama mkoa wa Shinyanga ambapo Shirika la Kitanzania lisilo la kiserikali la Ariel Glaser Pediatric Aids Healthcare Initiative(AGPAHI) linalojihusisha na mapambano dhidi ya Virusi vya UKIMWI na UKIMWI limefanya Bonanza la Michezo kwa vijana.Bonanza hilo limewakutanisha vijana 120 kutoka Vituo vya Afya vilivyopo katika halmashauri ya wilaya ya Ushetu,Msalala na Kahama Mji.


Bonanza hilo lililofanyika Jumamosi,Mei 21,2016 liliandaliwa na AGPAHI likiwezeshwa na Mfuko wa Kusaidia watoto wa Uingereza ( Children’s Investment Fund Foundation UK- (CIFF) limekutanisha vijana wenye umri kati ya miaka 15 hadi 19,ambao wapo katika rika balehe,rika ambalo ni muhimu sana katika jamii.



Mgeni rasmi katika Bonanza hilo la Michezo alikuwa Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa.Wengine waliohudhuria Bonanza hilo ni waganga wakuu wa halmashauri za wilaya ya KahamaMji,Ushetu na Msalala,wasimamizi wa klabu za vijana,vijana,wafanyakazi wa AGPAHI na wakazi wa Kahama.


Awali akisoma risala wakati wa Bonanza hilo,Mratibu Miradi kutoka AGPAHI, Dr. Amos Scott alisema shirika lake linajitahidi kuwashirikisha vijana wa rika balehe katika michezo na kuwapatia habari na elimu sahihi kuhusu huduma rafiki za afya ya uzazi katika maeneo mbalimbali ambako shirika linafanya shughuli zake.


“Bonanza hili la michezo linahusisha vijana 120 wanaotoka kwenye klabu 9 za vijana za Kituo cha afya Ushetu,Bulungwa,Ukune,Lunguya,Chambo,Chela,zahanati ya Kagongwa,Hospitali ya Mji wa Kahama na zahanati ya Segese zilizopo katika halmashauri za wilaya ya Ushetu,Msalala na Kahama Mji ambazo zinasimamiwa na AGPAHI kwa kushirikiana na halmashauri za wilaya husika”,alieleza Dr. Scott.


Alisema lengo la bonanza hilo la michezo ni kutoa burudani kwa vijana,kuleta furaha,matumaini na kujenga urafiki baina yao.


“Vijana hawa wanapokuwa katika klabu zao,tumekuwa tukiwapatia vitabu,vipeperushi,mikanda ya video na kadhalika ili kuwapatia elimu zaidi juu ya afya ya uzazi ,tunawasisitiza viongozi wa afya ngazi ya halmashauri za wilaya kuhakikisha kuwa vijana wanaendelea kupata elimu sahihi kuhusu afya ya uzazi ili waweze kufanya maamuzi sahihi”,aliongeza Dr. Scott.


Akifungua Bonanza hilo la Michezo, mkuu wa wilaya ya Kahama,Mheshimiwa Vita Kawawa alilipongeza shirika hilo kwa kuwajali vijana kwa kuwakutanisha ili wajifunze kupitia michezo.


“Natumia fursa hii kwa namna ya pekee kabisa kulishukuru shirika la AGPAHI kwa kuendelea kuwa karibu na hawa vijana,niwapongeze pia kuanzisha klabu za vijana ambao mmekuwa mkiwakutanisha kila mwezi ili wajifunze kwa pamoja masuala mbalimbali kama vile masuala ya rika kwa vijana na kushirikiana katika kutatua changamoto zao za afya ya uzazi na Virusi vya UKIMWI na UKIMWI”,alisema Kawawa.


Katika hatua nyingine Mheshimiwa Kawawa alitoa wito kwa viongozi wa halmashauri za wilaya husika kuendelea kutoa ushirikiano kwa shirika la AGPAHI hususani katika kutekeleza majukumu ya kuwasaidia wananchi katika huduma za afya hasa kwa watu wanaopata tiba na matunzo ili huduma zipatikane katika ubora na ziwe rafiki kwa wananchi.


Miongoni mwa michezo katika Bonanza hilo ni pamoja na mpira wa miguu,riadha,kuvuta kamba,kukimbia na mayai,kukimbiza kuku,kucheza muziki,kunywa soda kwa haraka zaidi,mbio za magunia na kuimba ambapo kila mshindi na washiriki wote walipatiwa zawadi hali iliyoongeza furaha zaidi kwa vijana hao.


Mwandishi wetu Kadama Malunde alikuwepo katika Bonanza hilo la Michezo kuanzia mwanzo hadi mwisho,ametuletea matukio katika picha. Fuatilia hapa….


Kabla ya Michezo Kuanza-Mratibu Miradi kutoka AGPAHI Dr. Amos Scott akisoma risala kwa mgeni rasmi (mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa) katika Bonanza la Michezo lililokutanisha vijana 120 kutoka vituo vya afya,zahanati na hospitali katika halmashauri za wilaya za Ushetu,Msalala na Kahama Mji mkoani Shinyanga

Vijana kutoka katika Halmashauri ya wilaya ya Ushetu,Kahama Mji na Ushetu wakiwa uwanjani kwa ajili ya Bonanza la Michezo lililoandaliwa na shirika la AGPAHI

Aliyesimama ni Mratibu Miradi kutoka AGPAHI Dr. Amos Scott akisoma risala kwa mgeni rasmi,ambaye ni mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa(kulia),kushoto ni Afisa Miradi Kutoka AGPAHI Sipemba Julius.Dr Scott alisema Bonanza hilo linatoa fursa kwa vijana kufurahi,kujifunza kushirikiana,kufahamiana na kupata marafiki

Aliyesimama ni Kaimu Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Mji Kahama Dr.George Masasi akimkaribisha mgeni rasmi Mheshimiwa Vita Kawawa (Kushoto),kulia ni Mganga mkuu wa halmashauri ya wilaya ya Msalala Dr. Hamidi Nyembea

Aliyesimama ni Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akifungua Bonanza la Michezo katika uwanja wa taifa mjini Kahama ambapo alilishukuru Shirika la AGPAHI kwa kuandaa Bonanza hilo huku akiliomba shirika hilo kuona umuhimu wa kuwasaidia vijana wenye vipaji katika michezo

Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akizungumza wakati wa kufungua Bonanza la Michezo ambapo aliwataka vijana kuonesha vipaji vyao pia kujifunza kupitia michezo

Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akiteta jambo na Kaimu Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Mji Kahama Dr.George Masasi (katikati)na Mganga mkuu wa halmashauri ya wilaya ya Msalala Dr. Hamidi Nyembea (kulia)

Bonanza ndiyo linaanza-Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akionesha kipaji chake cha kucheza na mpira wakati wa kukagua timu za mpira wa miguu za klabu za vijana kutoka halmashauri ya Mji Kahama,Ushetu na Msalala

Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akishikana mkono na wachezaji wa Timu ya Vijana kutoka Halmashauri ya Mji wa Kahama wakati wa kukagua timu hiyo

Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akishikana mkono na wachezaji wa timu ya mpira wa miguu ya vijana kutoka halmashauri ya Msalala

Wachezaji wa timu ya vijana kutoka halmashauri ya Ushetu wakifanya mazoezi kabla ya kuungana na vijana wa timu ya vijana kutoka halmashauri ya wilaya ya Msalala kuikabili timu ya vijana wa halmashauri ya wilaya ya Kahama Mji

Mkuu wa wilaya ya Kahama Vita Kawawa akiwaasa vijana kucheza mchezo wa amani.Mchezo huo wa mpira wa miguu ulikuwa kati ya Timu ya Vijana kutoka Halmashauri ya Ushetu walioungana na Vijana wa timu ya vijana kutoka halmashauri ya wilaya ya Msalala dhidi ya timu ya vijana wa halmashauri ya wilaya ya Kahama Mji.

Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akifungua Mchezo wa Mpira wa Miguu kwa penati aliyoielekeza kwa golikipa wa timu ya vijana kutoka Ushetu

Hata hivyo shuti kali la Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa liliishia kwenye mwamba

Kabla ya mchezo kuanza Mgeni rasmi Mheshimiwa Vita Kawawa na wafanyakazi wa AGPAHI wakapiga picha ya kumbukumbu

Mgeni rasmi Mheshimiwa Vita Kawawa akiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi kutoka halmashauri za wilaya ya Kahama Mji,Ushetu na Msalala pamoja na wafanyakazi wa AGPAHI na wachezaji timu ya vijana wa halmashauri ya Mji wa Kahama

Mgeni rasmi Mheshimiwa Vita Kawawa akiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi kutoka halmashauri za wilaya ya Kahama Mji,Ushetu na Msalala pamoja na wafanyakazi wa AGPAHI na wachezai timu ya vijana wa halmashauri ya Mji Msalala

Mchezo katia ya Msalala na Ushetu Vs Kahama Mji ukaendelea ambapo kipindi cha kwanza walicheza dakika 15 na kipindi cha pili dakika 15 na mpaka dakika 30 za mchezo zinamalizika Kahama Mji walijipatia magoli Matano huku Msalala na Ushetu wakiambulia pamoja na kwamba waliungana pamoja

Mchezo wa kukimbia na mayai nao ukachukua nafasi yake...ambapo Helena kutoka Kahama Mji (kushoto) aliibuka mshindi na kupata zawadi ya begi la shule

Shindano la Kuvuta kamba likaendelea...kati ya vijana kutoka Kahama Mji dhidi ya vijana wa Ushetu na Msalala,ambapo walitoka droo baada ya kamba kukatika

Mchezo wa kukimbia kwenye magunia nao ulikuwepo..Vijana wa Kiume kutoka Ushetu,Msalala na Kahama mji wanaonesha vipaji vyao.Katika mchezo huo Peter Kulwa kutoka Kahama Mji aliibuka mshindi na kupewa zawadi ya begi la shule

Vijana wa kike nao hawakuwa nyuma katika mchezo wa kukimbia kwenye magunia,ambapo Suzy John (katikati) kutoka Msalala aliibuka mshindi na kupewa zawadi ya begi la shule

Shindano la kufukuza kuku...ukimkamata anakuwa wako...

Kijana Faustine Daudi kutoka Msalala akiwa ameshikilia kuku wake baada ya kuwashinda wenzake

Kwa upande wa vijana wa kike Jesca Robert kutoka Kahama Mji akakamata kuku..alisikika akisema "Kesho nakula supu ya kuku huyu"

Shindano la Riadha/mbio za mita 100,pichani ni washindi kundi la wanaume..Wa kwanza ni Ibrahim Bure kutoka Kahama Mji,wa pili Oscar Onesmo kutoka Kahama Mji na wa tatu ni Faustine Daudi kutoka Msalala.Mshindi wa kwanza alipata zawadi ya saa ya mkononi.Kwa upande wa kundi la wasichana aliyeibuka mshindi ni Neema Bundala kutoka Msalala ambaye pia alipata zawadi ya saa ya mkononi

Shindano la kunywa soda kwa haraka kwa vijana wa kiume.Mshindi alikuwa Patrick Marco (kushoto) kutoka Msalala

Shindano la kunywa soda kwa haraka kwa vijana wa kike..Mshindi alikuwa Suzy John (katikati) kutoka Msalala

Shindano la kucheza muziki-Vijana wote wakaingia uwanjani kucheza muziki

Tunaangalia jinsi vijana wanavyocheza muziki...

Vijana wakicheza wimbo wa Alikiba "Nasema Nao"

Vijana wakiendelea kucheza muziki

Muda wa Kupeana Zawadi Ukawadia-Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akijiandaa kuanza kukabidhi zawadi kwa washindi katika michezo mbalimbali iliyochezwa uwanjani

Kulia ni Afisa Miradi Huduma Unganishi kwa jamii kutoka shirika la AGPAHI, Cecilia Yona akitoa maelezo kuhusu zoezi la utoaji zawadi kwa washindi katika Bonanza hilo

Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akimkabidhi zawadi ya begi la shule golikipa bora Damian Adam kutoka Ushetu

Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akimkabidhi zawadi ya begi la shule mfungaji bora wa mpira wa miguu Oscar Onesmo kutoka Kahama Mji

Mshindi wa shindano la kukimbia na mayai Grace kutoka Kahama Mji akishikana mkono na mratibu miradi kutoka AGPAHI Dr. Amos Scott

Mchezaji bora Paul George kutoka Ushetu akivaa saa aliyopewa ikiwa ni zawadi ya ushindi

Jesca Robert kutoka Kahama Mji akishikana mkono na Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa baada ya kuibuka mshindi katika mchezo wa kukimbiza kuku upande wa kundi la vijana wa kike

Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akimkabidhi zawadi ya saa ya mkononi neema Bundala kutoka Msalala aliyeshinda katika mbio za mita 100 kwa kundi la vijana wa kike

Vijana wakifuatilia zoezi la utoaji zawadi kwa washindi

Kijana Patrick Marco kutoka Msalala akiwa ameshikilia zawadi ya soda baada ya kuibuka mshindi katika shindano la kunywa soda kwa haraka zaidi upande wa kundi la vijana wa kiume

Kijana Suzy John kutoka Msalala akiwa ameshikilia zawadi ya soda baada ya kuibuka mshindi katika shindano la kunywa soda kwa haraka zaidi upande wa kundi la vijana wa kike


Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akikabidhi Kombe kwa Kapteni wa timu ya mpira wa miguu halmashauri ya Mji Kahama Oscar Onesmo kwa niaba ya vijana wote wa Kahama Mji.Kombe hilo lilitolewa kwa Halmashauri iliyoshinda michezo mingi zaidi kuliko halmashauri zingine

Wachezaji wa timu ya vijana kutoka Kahama Mji wakishangilia baada ya kukabidhiwa kombe la ushindi wa jumla

Vijana kutoka Kahama Mji wakiwa na kombe la ushindi wa jumla

Vijana na walezi wa vijana kutoka vituo mbalimbali vya afya wakiwa uwanjani wakishuhudia zoezi la utoaji zawadi


Vijana na walezi wa vijana katika vituo vya afya wakifuatilia kilichokuwa kinaendelea
Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akizungumza baada ya kumaliza kutoa zawadi kwa washindi katika bonanza hilo.
Mkuu huyo wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa pia alitoa zawadi ya pea moja ya soksi na kalamu kwa kijana aliyehudhuria bonanza hilo la Michezo

Mkuu wa wilaya ya Kahama Mheshimiwa Vita Kawawa akifunga bonanza la michezo ambapo aliwasisitiza vijana kusoma kwa bidii kwani elimu ndiyo ufunguo wa maisha

Picha ya pamoja-Mgeni rasmi MheshimiwaVita Kawawa,wafanyakazi wa AGPAHI,halmashauri za wilaya,walezi wa vijana katika vituo vya afya na vijana kutoka Halmashauri ya mji wa Kahama

Picha ya pamoja-Mgeni rasmi Mheshimiwa Vita Kawawa,wafanyakazi wa AGPAHI,halmashauri za wilaya,walezi wa vijana katika vituo vya afya na vijana kutoka halmashauri ya wilaya ya Ushetu

Picha ya pamoja-Mgeni rasmi Mheshimiwa Vita Kawawa,wafanyakazi wa AGPAHI,halmashauri za wilaya,walezi wa vijana katika vituo vya afya na vijana kutoka halmashauri ya wilaya ya Msalala

Vijana kutoka halmshauri ya Mji wa Kahama wakiwa katika picha ya pamoja na kombe lao

Vijana kutoka halmshauri ya Mji wa Kahama wakiwa katika picha ya pamoja na walezi wao na kombe lao wakiwa wao ndiyo wameshinda michezo mingi

Picha zote na Kadama Malunde-Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post