Vibaka Wa Pikipiki Wanusurika Kifo Kwa Kupigwa Mawe na Wananchi Baada ya Kukwapua Mkoba wa Mwanamke Huko Morogoro




Wananchi wenye hasira kali wamewapiga na kuwajeruhi vibaya watu wawili wanaodaiwa kufanya vitendo vya uporaji kwa kutumia pikipiki maarufu kama boda boda, ambapo watu hao wamenusuriwa kifo na kulazwa katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Morogoro kwa matibabu. 




Tukio hilo limethibitishwa na Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro Ulrich Matei ambaye amebainisha kuwa vijana hao waliotambuliwa kwa jina moja moja la Ngasa na Makirikiri wamejeruhiwa vibaya na wananchi kwa kupigwa mawe na magogo.


Amesema  walipigwa baada ya kumpora mkoba mwanadada Pendo Wilson mkazi wa Msamvu na kukimbia, wakati akitoka nyumbani kwake kuelekea kazini, ambapo waporaji hao waliofukuzwa na wananchi na kukamatwa, walikuwa kwenye pikipiki aina ya sanlg yenye namba za usajili T 436 AVX.

Hata hivyo kamanda Matei amewaasa wananchi kuacha kujichukulia sheria mikononi pindi wanapobaini matukio ya kiuhalifu, badala yake watoe taarifa kituo chochote cha polisi na mamlaka zingine za dola, na kuwashauri viongozi wa waendesha pikipiki kuunda vikundi na kutambuana ili kuwabaini wahalifu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post