Bilioni 1.3 Zimekusanywa Kutoka Daraja la Nyerere la Kigamboni


Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii ‘NSSF’ Prof. Godius Kahyarara ameeleza mapato yaliyopatikana kwenye daraja la Nyerere tangu lilipofunguliwa rasmi Mei 14, 2016.


Prof Kahyarara amesema jumla ya shilingi bilioni 1.3 zimekusanywa kutoka Daraja hilo lililopo Kigamboni jijini Dar es Salaam kupitia tozo mbalimbali zinazolipwa na vyombo vya usafiri vinavyopita darajani hapo.


Prof. Kahyarara ameongeza kuwa fedha hizo zimekusanywa kupitia tozo za magari yakiwemo magari binafsi, magari ya abiria, magari ya mizigo, pikipiki na bajaji zinazopita darajani hapo kila siku.


Kwa upande wake Msimamizi wa Mradi wa Daraja la Nyerere, Bw. Gerald Sondo alisema kuwa Serikali kwa kushirikiana na uongozi wa daraja wana mpango wa kuboresha huduma za malipo ili watumiaji wa daraja hilo waweze kulipa tozo kwa kutumia kadi za kielektroniki.


“Hivi karibuni tunatarajia kuanzisha mfumo wa malipo kwa kutumia kadi za kielektroniki ambapo madereva wa vyombo vya usafiri watakuwa wanatumia kulipa tozo pindi wanapopita darajani”.


Aidha alisema kuwa kwa sasa idadi ya magari, pikipiki na bajaji zinazopita darajani hapo ni kati ya elfu 8 hadi elfu 10 kwa siku na wanalipa tozo kulingana na aina ya chombo cha usafiri.


Akieleza kuhusu usalama wa daraja na watumiaji wake, Sondo alisema kuwa ulinzi ni wa uhakika kwa saa 24 kila siku kwani kuna askari wa kutosha pamoja na kamera zinazosaidia zoezi hilo pia kuwa wanaandaa kanuni za matumizi ya daraja ikiwemo faini za uharibifu, uchafuzi wa mazingira, matumizi mabaya ya njia na lugha za matusi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post