NACTE YAFUTA MATOKEO MITIHANI YA NADHARIA PROGRAMU YA UTABIBU NGAZI YA TANO



Na Dotto Kwilasa DODOMA.

BARAZA la Taifa la elimu ya ufundi (NACTE) limefuta matokeo ya mitihani ya nadharia kwa masomo yote ya programu ya Utabibu ngazi ya tano(NTL level 5) na kuagiza kurudiwa upya kwa mitihani hiyo ndani ya wiki sita kuanzia tarehe 1Novemba,2021.

Hatua hiyo imekuja kufuatia kuwepo kwa viashiria vya kuvuja kwa mitihani hiyo siku ya mwisho ya ufanyaji wa mitihani ya nadharia na hivyo kulazimika kuunda kamati ya uchunguzi iliyojumuisha wataalamu kutoka kwenye vyombo vya ulinzi na usalama.

Hayo yamesemwa leo Jijini Dodoma na Mganga Mkuu wa Serikali Aifello Sichalwe wakati akiongea na Waandishi wa habari kuhusu kuvuja kwa mitihani ya utabibu iliyofanyika mwezi 16 Augusti hadi 30 Septemba Mwaka huu na kueleza kuwa mitihani hiyo itafanyika sambamba na mitihani ya marudio Kwa programu nyingineza afya nchi nzima.

Kwa mujibu wa Dkt.Sichalwe kamati hiyo ilibaini kwamba mitihani ya mwaka wa pili ya programu ya Utabibu (Clinical Medicine)ilivuja lakini mitihani ya programu zingine haikuvuja.

"Wakati wa uchunguzi wa mitihani iliyovuja kamati ilibaini kuwa mitihani hiyo ilisambazwa kupitia mitandao ya kijamii na kuonekana kwenye baadhi ya namba za simu za wanafunzi zilizofanyiwa uchunguzi na kamati,",amefafanua Mganga Mkuu huyo wa Serikali.


Dkt. Sichalwe amesema,kwa kuwa Wizara ya afya inatambua umuhimu wa rasilimali watu wenye weledi na umahiri kwa ajili ya usalama wa afya za wananchi hivyo itaendelea kutoa ushirikiano kwa vyombo vya ulinzi na usalama ili kukamilisha uchunguzi na kuwachukukia hatua wadanganyifu wote.

Kutokana na umuhimu huo,kamati ya uchunguzi imewasilisha taarifa ya uchunguzi ambayo imethibitisha kuwepo kwa udanganyifu kwenye baadhi ya vyuo vilivyochunguzwa na kwamba uchunguzi zaidi unaendelea jubaini watu,Taasisi na vyuo vinavyojihusisha na udanganyifu wa mitihani .

"Taarifa hiyo imewasilishwa kwenye NACTE tarehe 24 Oktoba,2021 Kwa ajili ya maamuzi kwani ndicho chombo Cha kisheria chenye Mamlaka na vyuo vya elimu ya kati nchini,"amesema.

Dkt. Sichalwe alieleza kuwa Wizara ya afya inawaelekeza Wakuu wa vyuo vyote vya afya kuwapa taarifa wanafunzi ili wajiandae kwa ajili ya mitihani hiyo na kuwatahadharisha wanafunzi kuwa makini kwani mtaalamu wa afya aliyejipatia sifa kwa njia ya udanganyifu ni hatari kwa wananchi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
أحدث أقدم