



********************
Na Munir Shemweta, WANMM ARUSHA
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula ametaka kutengenezwa kwa mipango bora ya kusimamia ardhi kwa lengo la ardhi kubaki katika ubora wake wa matumizi yaliyokusudiwa kwa wanyama na binadamu.
Alisema, kutengenezwa kwa mpango wa matumizi bora ya kusimamia ardhi kutaisaidia jamii kwa ujumla pamoja na kutunzwa kwa ardhi kwa ajili ya vizazi vijavyo.
Dkt Mabula alisema hayo Julai 1, 2022 katika Kituo cha Urtithi wa Utamaduni mkoani Arusha wakati aliposhiriki Maadhimisho ya Miaka 60 ya Mfuko wa Wanyamapori wa Afrika (Africa Wildlife Foundation). Maadhimisho hayo yaliambatana na Maonesho ya Tuzo za Picha zilizopewa jina la Rais Mstaafu wa Serikali ya Awamu ya Tatu Benjamin William Mkapa (Benjamin Mkapa African Wildlife Awards).
‘’Mipango bora ya usimamizi wa ardhi inaweza kutusaidia sisi wenyewe na kutunzwa ardhi kwa ajili ya vizazi vijavyo na haya yote ni jukumu letu kutunza ili kurithisha vizazi vijavyo’’. Alisema Dkt Mabula
Kwa mujibu wa Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, wizara yake inayo furaha kufanya kazi na jamii ikiwemo Mfumo wa Wanayamapori wa Afrika katika juhudi za kusimamia rasilimali kwa manufaa ya binadamu na wanyamapori.
Alitaka washiriki wa maadhimisho hayo kujiuliza namna watakavyoweza kushiriki katika kuhakikisha mazxingira yanakuwa salama, ardhi inatunzwa sambamba na kupangiwa matumizi mazuri ya kuishi binadamu na wanyama bila kuleta taharuki..
Kwa upande wake Rais Mtaafu wa serikali ya awamu ya nne Jakaya Mrisho kikwete aliyekuwa mgeni rasimi kwenye maadimisho hayo, aliupongeza Mfuko wa Wanayamapori wa Africa kwa kutimiza miaka 60 tangu kuanzishwa kwake na kueleza kuwa mfuko huo umefanya mambo mengi katika masuala ya utunzaji mazingira na wanayama na kutaka kazi hiyo iendelee.
Alisema, pamoja na kufurahishwa na maonesho yaliyohudhuriwa pia na famialia ya Mkapa akiwepo Mama Mkapa lakini kilichomfurahisha zaidi ni tuzo za picha za wanayamapori kupewa jina la Rais huyo Mstaafu wa serikali ya awamu ya tatu ambapo alisema uamuzi huo ni ishara nzuri ya juhudi zilizofanya na Mkapa katika usimamizi wa mazingira na kueleza kuwa tuzo hizo zitakuwa zikikumbusha utunzaji mazingira na wanyamapori.
‘’Nimefurahishwa sana na picha hii ni juhudi kubwana kilichonifurahisha kikubwa ni tuzo zinaitwa Benjamin Mkapa African Wildlife, hii ni faraja kubwa sana’’ alisema Jakaya Mrisho Kikwete.
Social Plugin