TANZANIA NA ZANZIBAR ZASAINI HATI YA MAKUBALIANO SEKTA YA MADINI




Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko ameshuhudia utiaji saini wa Hati ya Makubaliano kati ya Wizara ya Madini ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Wizara ya Maji, Nishati na Madini ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Makubaliano hayo ni mwendelezo wa ushirikiano uliopo baina ya wizara hizo mbili zilizopo katika upande wa Muungano ikiwa ni maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa Februari, 2023 jijini Arusha ya kushirikiana kwa lengo la  kufanya madini yaliyopo katika maeneo husika yaweza kuleta manufaa kwa pande zote mbili.

Katika hafla hiyo iliyofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa ofisi ndogo ya Wizara ya Madini jijini Dar es Salaam Dkt. Biteko amewataka watendaji wa wizara hizo kusimamia utekelezaji wa makubaliano 

"Maelekezo ya Mheshimiwa Rais yalitupa dira mpya katika kuendeleza mashirikiano yetu, hivyo tulichosaini leo sio kwa ajili ya kupiga picha bali ni kwa ajili ya kazi tuliyojipatia, natamani kuona mambo tuliyosaini hapa yanakuwa mfano na yanafanyika kwa weledi kwa ajili ya manufaa ya pande zote mbili," amesema Dkt. Biteko.

Aidha, Dkt. Biteko amewataka watendaji wakuu wa pande zote mbili kusimamia masuala hayo ili  yaweza kutokea huku akitaka kuanza kusimamia masuala ambayo hayahitaji rasilimali fedha kubwa ikiwemo kufanya tafiti hivyo yale yanayowezeka yaanziwe kufanyiwa kazi leo na sio kungoja.

Pia, amewataka Makatibu Wakuu wa pande zote mbili kutengeneza timu ndogo ya kusimamia makubaliano hayo ili kuhakikisha ushirikiano huo unadumu na kuwa wa mafanikio katika pande hizo mbili.

Naye, Waziri wa Maji, Nishati na Madini Shaibu Hassan amesema utiaji wa saini wa makubaliano hayo usiishie kwenye makaratasi bali ufanisi na utendaji unaotakiwa kuonekana ukaonekane.

"Kitendo kinachofanyika leo ni kitendo muhimu sana kwa kwa pande zote mbili ambapo viongozi wetu wa juu wamekuwa wakitusisitiza kuendeleza mashirikiano ambapo tunategemea kushirikiana hasa katika suala la utaalamu hususan katika kufanya tafiti kwa pamoja," amesema Hassan.

Pia, Hassan amesema ushirikiano huo utazaa toka kwa pande zote mbili za muungano na kuwataka watendaji wa wizara yake kufanya kile kinachowezekana kunyika leo na wasingoje kesho. 

Jumla ya Hati Tano za Makubaliano zimesaniwa kwa taasisi zote zilizo chini ya wizara ambazo ni Tume ya Madini, Taasisi ya Uwazi na Uwajibikaji katika Rasilimali Mafuta, Madini na Gesi Asilia, Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) pamoja na Kituo cha Jemolojia na Tanzania (TGC).

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post