HALMASHAURI YA TANDAHIMBA YAZINDUA MAADHIMISHO YA WIKI YA UNYONYESHAJI


Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii Halmashauri ya Wilaya ya Tandahimba Ndg.Aloyce Massau Agosti 4,2023 amezindua rasmi maadhimisho ya Wiki ya unyonyeshaji duniani katika Hospitali ya Wilaya ya Tandahimba kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi uliofanyika katika hospitali ya Wilaya amesema kuwa Unyonyeshaji wa maziwa ya mama ukifanyika ipasavyo watoto wachanga watakuwa na hali nzuri ya lishe itakayoboresha ukuaji na maendeleo ya kimwili na kiakili

Aidha amesema kuwa Unyonyeshaji ukizingatiwa gharama za matibabu zitapungua kutokana na kuimarika kwa kinga ya mwili kwa watoto hali itakayosababisha kupungua kwa kasi ya watoto kuugua mara kwa mara

" Maadhimisho haya yawe chachu ya kuchochea mabadiliko chanya ya kilishe ili kujenga,kukuza na kusaidia unyonyeshaji," amesema Massau

Kwa upande wake Mganga Mkuu Hospitali ya Wilaya ya Tandahimba Dkt.Grace Paul amewasistiza akina mama kuzingatia taratibu sahihi za unyonyeshaji ambazo wanapewa na wataalamu katika vituo vya kutolea huduma

"Maadhimisho haya katika Halmashauri yetu tumeanza kuanzia Agosti 1, ambapo elimu inatolewa kwa jamii,muhimu akina mama kuzingatia elimu wanayopewa ma wataalamu",amesema Dkt.Grace

Naye Afisa Lishe Tandahimba, bwana Innocent Mbwaga amewasisitiza akina mama kunyonyesha watoto wao kwa upendo, kwani ndio msaada wao wa baadae na Taifa kwa ujumla.

Aidha ,Afisa lishe huyo amesema ni lazima "mtoto anyonye maziwa ya mama tu, kwa muda wa Miezi 6, bila kuchanganya hata na maji,kwani Maziwa ya mama yana kila kirutubisho"

Maadhimisho ya Wiki ya Unyonyeshaji Duniani hufanyika kila Mwaka ambapo kauli mbiu ya Mwaka huu " Saidia Unyonyeshaji,wezesha Wazazi kulea Watoto na kufanya kazi zao kila siku"

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post