SEED SCIENCE YATOA VIFAA SHULE ZA MSINGI NA SEKONDARI PWANI NA MOROGORO

Afisa Elimu Sekondari halamashauri ya Chalinze Mwl. Salama Ndetabula akikabidhi kasha la vifaa vya sayansi kwa walimu wa shule ya msingi Mboga  jana.

NA. ELISANTE KINDULU, CHALINZE

MRADI wa Seed Science umetoa makasha  ya vifaa vya sayansi kwaajili ya baadhi ya shule za msingi na Sekondari katika halmashauri ya Chalinze mkoa wa Pwani na halmashauri ya Morogoro vijijini katika mkoa wa Morogoro vyenye thamani ya shilingi milioni 1.6.

Vifaa hivyo vilikabidhiwa Jana kwenye shule 8 za halmashauri hizo mara baada ya maonyesho ya ubunifu na matumizi ya zana za sayansi kutoka kwa wanafunzi katika ukumbi wa Magereza, Bwawani mjini hapa.

Shule zilizonufaika na vifaa hivyo ni pamoja na Shule za Msingi za Kibiki, Msolwa, Mboga, Mdaula "B" na Shule ya Sekondari Mboga, zote kutoka hamashauri ya Chalinze.

Kutoka Morogoro vijijini, shule zilizopokea vifaa hivyo ni shule za Sekondari za Fulwe, Mikese na Nelson Mandela.

Akikabidhi vifaa hivyo kwa walimu mara baada ya kupokea kutoka katika mradi huo, Afisa Elimu Sekondari wa halmashauri ya Chalinze Bi. Salama Ndyetabula alimpongeza mwanzilishi wa shirika hilo Bw. Michelle Ragio na washirika wake kwa msaada huo, Kwani utarahisisha ufundishaji na utasaidia kuinua taaluma za wanafunzi katika kujifunza.

Bi. Salama  pia aliwapongeza walimu kwa juhudi zao za kuibua vipaji vya wanafunzi na kuwashauri walimu hao wawe wanashirikisha wanafunzi katika mashindano ya ubunifu yanayotangazwa na taasisi mbalimbali nchini ili kuendeleza vipaji vya wanafunzi wao. 

Maonyesho hayo na utoaji wa vifaa hivyo ulihudhuriwa pia na mkurugenzi wa Ngeriver Eco- Camp, Bw. Remigius Mushenga, Mratibu wa mafunzo wa mradi huo Mwl. Joseph Laurent, Diwani wa kata ya Ubena Mh. Geofrey Kamugisha, Wakuu wa shule za Sekondari za Mdaula, Ubena Bwawani pamoja na shule zingine zilizopo kwenye mradi huo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post