MTOTO MWENYE UALBINO ALIYECHUKULIWA NA WATU WASIOFAHAMIKA AKUTWA AMEUAWA, VIUNGO VIMEKATWA


Mtoto Asimwe Novath enzi za uhai wake
Mwili wa mtoto Asimwe Novath ukipakizwa kwenye gari

Na Mariam Kagenda _ Kagera 

Mwili wa mtoto mwenye Ualbino  Asimwe Novath  ambaye  alichukuliwa na watu wasiofahamika  nyumbani kwao  katika kijiji cha Bulamula kata ya Kamachumu wilayani Muleba Mkoani Kagera umekutwa ukiwa umetupwa kwenye karavati na kuondolewa baadhi ya viungo vyake vya mwili katika kijiji cha Marere kata ya Ruhanga wilaya ya Muleba.

Akizungumza leo Juni 17,2024 baada ya kupatikana kwa Mwili huo katibu tawala wilaya ya Muleba Bwana Benjamini Mwikasyege amesema kuwa wamepata taarifa majira ya asubuhi kutoka kwa wasamaria wema walioona mwili huo na baada ya kufika katika eneo hilo walikuta mwili  ukiwa umetupwa kwenye Karavati na umekatwa mikono.


Amesema kuwa mwili wa mtoto huyo umepelekwa Mochwari na Jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi na baada ya uchunguzi  watazungumza na familia ya mtoto  kwa ajili ya kumstiri mtoto huyo katika nyumba yake ya milele.


Mtoto huyo aliyekuwa na umri wa miaka 2 na nusu alichukuliwa na watu wasio fahamika nyumbani kwao Mei 30 mwaka huu Majira ya saa moja jioni baada  ya watu wawili kuja kuomba msaada wa chumvi kwa mama wa mtoto huyo kisha kumkaba na kuchukua mtoto

Kwa upande wake Afisa mtendaji wa kata ya Ruhanga amesema kuwa alipigiwa simu na mwenyekiti wa kijiji cha Marere kuwa kuna mwili wa mtoto umepatikana katika kijiji hicho ukiwa umetupwa kwenye Karavati hivyo akafanya mawasiliano ngazi ya wilaya na ndugu wa marehemu.

Amesema kuwa katika kata hiyo tukio kama hilo halijawahi kutokea ambapo amewahimiza wananchi kujiepusha na vitendo vya ukatili kwani watu wenye ualbino wanatakiwa kuishi kama ilivyo kwa watu wengine .

Nao baadhi ya wananchi wa kijiji cha Marere kata ya Ruhanga wamelaani kitendo hicho na kuliomba Jeshi la polisi kuwatafuta watu waliohusika na kitendo hicho ili wafikishwe kwenye vyombo vya Sheria .

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post