EWURA YAZINDUA RIPOTI YA UTENDAJI WA SEKTA ZA NISHATI


Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko (WA Nne kushoto) akiwa ameshika taarifa za utendaji katika Sekta ndogo ya Umeme, Gesi Asilia na Mafuta kwa mwaka 2022/2023 mara baada ya kuzizindua jijini Dodoma. Wa tatu kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule na wa Nne kutoka kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba.

Na Alex Sonna-DODOMA

NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amezindua taarifa za utendaji katika Sekta ndogo ya Umeme, Gesi Asilia na Mafuta kwa mwaka 2022/2023 huku akiipongeza EWURA kwa tathmini ambayo inaonesha kuwa Sekta ya Nishati inaendelea kuimarika.

Akizindua taarifa hizo leo 14 Juni, 2024 jijini Dodoma, Dkt. Biteko,amesema kuwa EWURA imekuwa ikifanya kazi yake kwa weledi mkubwa katika kuimarisha sekta ya Nishati.

Dkt.Biteko ameipongeza EWURA kwa tathmini ambayo inaonesha kuwa Sekta ya Nishati inaendelea kuimarika, akitolea mfano kutolewa kwa leseni ya kuchimba gesi asilia katika kisima cha Ntorya kilichopo mkoani Mtwara kitakachotoa gesi futi za ujazo milioni 140 kwa siku ambapo leseni ya mwisho ya kuchimba gesi ilitolewa mwaka 2006.

“ Niwasisitize EWURA mhakikishe kuwa, tathmini ya mwaka ujao ihusishe utendaji wa Nishati Safi ya kupikia ili kuweza kujipima kwa usahihi kuhusu utekelezaji wa ajenda hii inayopewa kipaumbele na Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan.” Amesema Dkt. Biteko

Dkt. Biteko pia ameitaka EWURA kupima uhusiano wa rasilimali zilizopo na mafanikio ya watu ambapo amesisitiza kuwa mafanikio ya sekta lazima yaendane na mabadiliko ya maisha ya watu.

Hata hivyo ametoa maelekezo mahsusi kwa Wizara na Taasisi mbalimbali kufanyia kazi taarifa hizo zinazoonesha mafanikio na changamoto katika Sekta Nishati.

"Naagiza Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati pamoja na Wizara ya Mipango na Uwekezaji kusoma taarifa hizo na kuzichambua na changamoto zilizoainishwa zipatiwe majawabu ndani ya kipindi cha miezi mitatu."amesema

Aidha ameagiza kuwa, kila aina ya fursa iliyoonekana kwenye taarifa hizo ichukuliwe kwa uzito mkubwa na itambuliwe nani ana uwezo wa kuitumia fursa hiyo ndani ya Serikali na katika taasisi binafsi.

Pia ametaka mifumo ya uagizaji mafuta iendelee kuboreshwa baada ya kufanyika utafiti wa kina na kueleza kwamba miundombinu ya mafuta bado inahitajika huku akisisitiza kuwa urasimu usiwepo kwenye Sekta ya Nishati.

Kuhusu sekta ndogo ya umeme amesema amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kuiboresha ambapo leo ametoa taarifa kuwa mradi wa Julius Nyerere (JNHPP) umeingiza mtambo wa pili katika gridi ya Taifa kupitia mtambo namba 8 na hivyo kufanya mradi huo kuingiza megawati 470 katika gridi.

“Sekta binafsi imetutoa kimasomaso, Serikali haiwezi kufanya kila kitu, wamefanya kazi kubwa mno kwenye mafuta, gesi na hata kwenye uzalishaji umeme, wito wangu kwenu msibaki nyuma changamkieni fursa, na kwa taasisi zilizo chini ya Wizara msione sekta binafsi kama watu wajanjawajanja, tuwape kipaumbele.” amesema Dkt. Biteko

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba amesema kuwa katika tathimini iliyozinfuliwa inaonesha sekta imepiga hatua kwenye maeneo megi ikiwemo uhakika wa upatikanaji umeme, upatikanaji na usambazaji wa mafuta kuimarika hasa baada ya Dkt. Doto Biteko kuanza kuongoza Wizara ya Nishati.

"Upatikanaji na uwekezaji wa gesi unaendelea kuimarika na hii ikijumuisha usambazaji gesi kwenye maeneo mbalimbal .kama magari, majumbani na viwandani."amesema

Naye Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amemshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuiimarisha Sekta ya Nishati na kusema kuwa Dodoma imeshuhudia matunda ya uimarishaji huo wa sekta kwani sasa umeme haukatiki.

Awali akitoa taarifa za utendaji katika Sekta ya Nishati, Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dkt. James Andilile alisema kuwa Sekta ya Nishati inaendelea kuimarika ikiwemo uwekezaji kwenye miundombinu ya mafuta, uwekezaji wa vituo vya mafuta na maghala umeongezeka, kuna ongezeko la uagizaji wa Gesi ya Mitungi (LPG) kwa asilimia 16 na ongezeko la uagizaji wa mafuta kwa asilimia 8.

"Katika Sekta ya umeme uwekezaji umeongezeka katika uzalishaji, usafirishaji na usambazaji, upotevu wa umeme unazidi kupungua na wateja wa umeme wameongezeka kutoka milioni 3.8 mwaka 2021/22 hadi milioni 4.4 mwaka 2022/2023."amesema Dkt.Andilile


NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko,akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa taarifa za utendaji katika Sekta ndogo ya Umeme, Gesi Asilia na Mafuta kwa mwaka 2022/2023,iliyofanyika leo Juni 14,2024 jijini Dodoma.


KATIBU Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba,akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa taarifa za utendaji katika Sekta ndogo ya Umeme, Gesi Asilia na Mafuta kwa mwaka 2022/2023,iliyofanyika leo Juni 14,2024 jijini Dodoma.


Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dkt. James Andilile ,akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa taarifa za utendaji katika Sekta ndogo ya Umeme, Gesi Asilia na Mafuta kwa mwaka 2022/2023,iliyofanyika leo Juni 14,2024 jijini Dodoma.


KAIMU mhe. angelina mabula, kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini,Mhe.Angelina Mabula,akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa taarifa za utendaji katika Sekta ndogo ya Umeme, Gesi Asilia na Mafuta kwa mwaka 2022/2023,iliyofanyika leo Juni 14,2024 jijini Dodoma.

MAKAMO Mwenyekiti wa Bodi ya EWURA Bi.Victoria Elangwa,akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa taarifa za utendaji katika Sekta ndogo ya Umeme, Gesi Asilia na Mafuta kwa mwaka 2022/2023,iliyofanyika leo Juni 14,2024 jijini Dodoma.


Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule,akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa taarifa za utendaji katika Sekta ndogo ya Umeme, Gesi Asilia na Mafuta kwa mwaka 2022/2023,iliyofanyika leo Juni 14,2024 jijini Dodoma.


Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu,akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa taarifa za utendaji katika Sekta ndogo ya Umeme, Gesi Asilia na Mafuta kwa mwaka 2022/2023,iliyofanyika leo Juni 14,2024 jijini Dodoma.


SEHEMU ya washiriki wakimsikiliza Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko (hayupo pichani) ,akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa taarifa za utendaji katika Sekta ndogo ya Umeme, Gesi Asilia na Mafuta kwa mwaka 2022/2023,iliyofanyika leo Juni 14,2024 jijini Dodoma.


Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko (WA Nne kushoto) akiwa ameshika taarifa za utendaji katika Sekta ndogo ya Umeme, Gesi Asilia na Mafuta kwa mwaka 2022/2023 mara baada ya kuzizindua jijini Dodoma. Wa tatu kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule na wa Nne kutoka kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba.


Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko akishuhudia utiaji Saini mkataba wa utendaji kazi kati ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) jijini Dodoma. Wanaotia Saini ni Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Gissima Nyamo-Hanga (kushoto) na Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dkt. James Andilile.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post