MRUTU AGRO YAWEZESHA VIJANA 30,000 KILIMO BIASHARA

Mkurugenzi mtendaji wa kampuni ya Mrutu Agro solutions Philipo Mrutu akizungumza mbele ya waandishi wa habari (hawapo pichani). 

Na Christina Cosmas, Morogoro

KAMPUNI inayojihusisha na kuuza bidhaa za kilimo na mifugo nchini Mrutu Agro-Solutions imefanikiwa kutoa elimu ya kilimo ujasiriamali kwa wakulima vijana zaidi ya 30,000 kati ya Milioni 10 wanaotakiwa kufikiwa ili kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa ajira na kipato nchini.

Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo Philipo Mrutu amesema kupitia kitengo cha smart Agri-preneurship innovation Centre wanahamasisha ujasiriamali katika kilimo kwa kuwajengea uwezo watu mbalimbali ikiwemo wanaomaliza masomo ili kutumia fursa zinazowazunguka katika kuzalisha kwa kujiajiri na kuajiri wengine na kujipatia kipato.

Alisema ipo changamoto ya watu kutotambua uwepo wa kilimo biashara na kufanya kilimo cha mazoea ambacho hakiwasaidii kama wakulima ambapo wakizingatia kanuni za kilimo biashara wanaweza kuona fursa zilizopo kwenye mnyororo wa thamani.

“Tunaweza kuwaunganisha wakulima na masoko lakini pia kupata huduma zote za kilimo biashara kuanzia kwenye kupata pembejeo nzuri, ushauri, teknolojia na kufanya kilimo kama biashara” alisema.

Akizungumzia changamoto ya mabadiliko ya tabianchi Mrutu aliwataka wakulima kuhamasika na kutumia kilimo kinachoitwa ‘Smart Agriculture’ kwa kutumia eneo dogo na kuzalisha kwa tija kwa kilimo kilicho himilivu na chenye kuzingatia ukijani katika kufanya kilimo mseto kwa kutumia njia za umwagiliaji, sola na kuendana na mazingira halisi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post