NAIBU WAZIRI WA NISHATI MHE. JUDITH KAPINGA AMEANZA ZIARA YA KIKAZI NDANI YA WILAYA YA KAHAMA


Na Mwandishi wetu _ Malunde 1 blog 

Naibu waziri wa Nishati Nchini Mheshimiwa Judith Kapinga ameanza ziara yake ya kikazi mkoani Shinyanga yenye lengo la kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali inayotekelezwa mkoani humo.

Ziara hiyo imeanza leo Julai 01, 2024 ndani ya halmashauri ya Ushetu wilayani Kahama na kutarajia kutamatika ifikapo Julai 03, 2024 ndani ya manispaa ya Kahama.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa jimbo la Ushetu Mbunge wa Jimbo hilo Mhe. Emmanuel Cherehani amesema Jimbo la Ushetu lina vitongoji 524 ambapo bado kuna baadhi ya maeneo hawajafikiwa na huduma ya umeme hivyo kumuomba mkandarasi kuongeza kasi ya utekelezaji.

“Jimbo la Ushetu lina kata 20 na Vitongoji 524 lakini bado kuna baadhi ya maeneo hawajafikiwa na umeme nikuombe Mheshimiwa naibu waziri wa Nishati wananchi hawa wamesubiri kwa muda mrefu lakini mpaka leo bado hawajasogezewa huduma ya umeme hali hii inasababisha shughuri za maendeleo kukwama kwenye baadhi ya maeneo”, amesema Chereheni.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo alipotembelea kijiji cha Sunga kata ya Uyogo halmashauri ya Ushetu Naibu waziri wa Nishati Nchini Mheshimiwa Judith Kapinga amemtaka mkandarasi anayetekeleza usambazaji wa umeme wilayani Kahama kupitia kampuni ya Tontan Project Technology Co. Ltd Jv Group Six International kueleza ni lini atamaliza utekelezaji wa mradi huo kwenye vijiji vyote ndani ya wilaya ya Kahama.

Akijibu swali hilo Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Tontan Project Technology Co. Ltd Jv Group Six International, John Zheng amesema ifikapo Julai 10 mwaka huu wanatarajia kukamilisha usambazaji wa umeme kwenye vijiji vyote ambavyo bado havijafikiwa na huduma ya umeme.

Aidha Mheshimiwa Judith Kapinga ametoa wito kwa wananchi kuendelea kutunza miudombinu ya umeme ili iweze kudumu kwa muda mrefu na kwa manufaa ya vizazi na vizazi lakini pia kujiunganishia umeme kwenye maeneo ambayo tayari yamekwishafikiwa na huduma hiyo.

Akizungumza kwa niaba ya serikali ya mkoa kaimu Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Wakili Julius Mtatiro ambaye pia ni mkuu wa wilaya ya Shinyanga amesema serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan imetoa fedha nyingi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo usambazaji wa umeme maeneo ya vijijini kupitia Wakala wa Nishati Vijijini REA.

Katika ziara hiyo ya kikazi ya Naibu waziri wa Nishati Nchini Mheshimiwa Judith Kapinga pia ametembelea katika Kijiji cha Nimbo kilichopo kata ya Chona pamoja na kijiji cha Nyawishi kata ya Chambo ndani ya halmashauri ya Ushetu.

 

Naibu waziri wa Nishati Nchini Mheshimiwa Judith Kapinga akiwasili ndani ya mkoa wa Shinyanga.

Naibu waziri wa Nishati Nchini Mheshimiwa Judith Kapinga akizungumza wakati wa ziara yake ndani ya Halmashauri ya Ushetu.

Naibu waziri wa Nishati Nchini Mheshimiwa Judith Kapinga (KUSHOTO) akiwa na kaimu mkuu wa Mkoa wa Shinyanga ambaye pia ni mkuu wa wilaya ya Shinyanga Julius Mtatiro.


Mbunge wa jimbo la Ushetu Emmanuel Cherehani akizungumza wakati wa ziara hiyo.



Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga ambaye pia ni mkuu wa wilaya ya Shinyanga Julius Mtatiro akizungumza wakati wa ziara hiyo.




Mwakilishi wa Mkurugenzi mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini REA ambaye pia ni Msimamizi wa Miradi Mhandisi Romanus Lwena akizungumza wakati wa ziara hiyo.

Mkandarasi kutoka Kamuni ya Tontan Project Technology Co. Ltd Jv Group Six International akizungumza wakati wa ziara hiyo.

Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Tontan Project Technology Co. Ltd Jv Group Six International, John Zheng akizungumza wakati wa ziara hiyo.

Baadhi ya wananchi wakizungumza wakati wa mkutano wa hadhara.

Baadhi ya wananchi waliojitokeza kwenye mkutano wa hadhara kata ya Chona.




Baadhi ya wananchi waliojitokeza kwenye mkutano wa hadhara kata ya Chambo.



Meneja wa Shirika la umeme Tanzania TANESCO Mkoa wa Shinyanga Mhandisi Leo Mwakatobe akizungumza wakati wa ziara hiyo.




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post