MZUMBE YABUNI MBEGU YA MGOMBA KUPITIA NDIZI MBIVU


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

KUFUATIA changamoto kwa wakulima wa zao la ndizi kuwa na uhaba wa mbegu bora za migomba ya ndizi, mwanafunzi wa Chuo Kikuu Cha Mzumbe amefanya utafiti na kubuni mbegu bora ya kisasa kwa kutumia ndizi mbivu ,

Akizungumza leo Julai 10,2024 katika Maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba yanayofanyika katika Viwanja Vya Mwalimu Nyerere, barabara ya Kilwa Jijini Dar es Salaam, Mwanafunzi wa Chuo Kikuu Mzumbe ndaki ya Mbeya, Bw. Gerald Mabuto amesema mbegu hiyo inahimili changamoto za magonjwa na huleta uzalishaji mkubwa wa muda mfupi kwani wanaweka madini ya Calcium ambayo husaidia kupambana na magonjwa.

Aidha Mabuto amesema kuwa mbegu katika hatua ya uoteshaji hadi kuota inatumia kipindi cha siku 15 hadi 18 ambapo siku 30 hadi 35 inakuwa tayari kwenda shambani.

Pamoja na hayo ameeleza kuwa mbegu hiyo inatoa matunda mazuri ambapo kwa wakulima walioichukua awali wameipenda kwani wameona faida yake .

"Baada ya kufanya utafiti wa mbegu hii, niliigawa kwa baadhi ya wakulima bure ili nijue matokeo yake, baadae walikuja na majibu kuwa mbegu hiyo ni bora kuliko mbegu ambazo wmekuwa wakizitumia ambazo huchukua muda mrefu mpaka uzalishaji" amesema 

Mabuto amesema mbegu hiyo inapatikana kwa oda maalumu kwa kipindi hiki ambapo bado anafanya taratibu za kibali.
Mwanafunzi wa Chuo Kikuu Mzumbe Ndaki ya Mbeya Bw. Gerald Cosmas Mabuto akielezea kuhusu ubunifu wake wa Kupanda migomba kwa kutumia ndizi mbivu asilia kama mbegu kwa baadhi ya watu waliotembelea banda la Chuo Kikuu Mzumbe

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post