RUWASA YATOA MAFUNZO YA UKUSANYAJI WA FEDHA ZA SERIKALI KWA MFUMO WA KIELEKTRONIKI WATOA HUDUMA ZA MAJI TANGA

Na Hamida Kamchalla, TANGA.

WAKALA wa Maji Vijijini na Usafi wa Mazingira (RUWASA) imewawezesha watoaji wa huduma ya maji ngazi ya jamii mkoani Tanga kwa kuwapa mafunzo ya ukusanyaji wa fedha za serikali kwa mfumo wa kielektroniki wa utoaji ankara za maji.

Katika ufungaji wa mafunzo hayo, watoa huduma hao wametakiwa kufanya kazi kwa weledi na kutatua kero za wateja bila kusababisha vikwazo baina yao.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi, Dkt. Batilda Buriani ametoa wito huo wakati akifunga mafunzo ya mfumo wa malipo ya pamoja wa serikali wa ankara za maji yaliyofanyika kwa siku 15 mkoani humo.

Dkt. Buriani amebainisha kwamba mfumo wa kielektroniki ni njia nzuri na ina manufaa makubwa endapo tu itatumika ipasavyo katika jambo husika na kuleta tija katika ukusanyaji wa fedha za serikali.

"Uzuri wa mitandao una faida kubwa sana, hivyo twende tukaitue vizuri kwa kuitumia kwa kutoa huduma nzuri kwa watu wetu, kuna muda unaweza ukatuma ujumbe kumbe simu haipo hewani, hivyo kwa sasa tunavyoanza twende na vitu vyote viwili,

"Tutume ujumbe lakini pia tuwe tunapitia kufuatilia majumbani kuhakikisha kama ujumbe umefika kwa muhisuka na mtakuwa mnapunguza kazi kubwa sana katika kuhakikisha fedha za serikali zinakusanywa, lakini vilevile huduma zinaboreshwa" amasema.

Lakini pia Dkt. Buriani ametoa wito kwa wananchi wote ambao ni watumiaji wa huduma ya maji wanapaswa kutimiza wajibu wao lakini pia kutoa agizo kwa Taasisi ambazo maeneo zilizopo hazitakiwi kulipia kwa maana ya maeneo mahususi ya serikali kama kwenye majeshi.

"Nitumie fursa hii kwa watuaji wote wa maji, kwa hakika ni wajibu wa kila mmoja wetu kulipa maji, kwa zile Taasisi ambazo hazilipi maji katika maeneo mahususi ambayo zimepangwa zisilipe hii haina shida" amebainisha.

"Kwamaana kama mimi nikiamua kwenda kuishika eneo ambalo ni nje na makazi niliyopangiwa ni lazima nilipe, hivyo niwaombe wote waliopo kwenye Taasisi ambazo wapo nje ya maeneo yao, tuwasaidie kulipa hizi bili ili isilete shida kwao katika ukusanyaji" amesema.

Meneja wa RUWASA Mkoa wa Tanga Upendo Lugongo amesema jumla ya watoa huduma hao wamepatiwa mafunzo ambayo yanahusisha maduhuli ya ukusanyaji wa fedha katika sekta ya maji vijijini.

Lugongo amefafanua kwamba mijini zipo Mamlaka za maji lakini vijijini kuna vyombo vya huduma za maji na katika Mkoa wa Tanga vipo vyombo 46 ambayo vinafanya kazi.

"Mafunzo haya yanaenda kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa maduhuli katika vyombo vya watumiaji wa maji, lakini kikubwa zaidi kuona fedha ambazo zinakusanywa ni sehemu ya fedha za serikali na zinatakiwa zisome kwenye mfuko wa serikali,

"Na zijulikane ni kiasi gani zinakusanywa kutoka kwenye maduhuli yanayokusanywa kutoka kwenye huduma za maji vijijini, ili kuona miradi ambayo imejengwa na serikali au Kwa kuwekeza Kwa fedha nyingi sana inaenda kuwa endelevu" amesema.

Pia Lugongo amesema mafunzo hayo yamewahusisha wananchi wanaoishi vijijini katika Mkoa huo ambapo baada ya mafunzo watakwenda kukusanya maduhuli kwa kuitumia mfumo wa kielektroniki na watalipia kupitia mawakala wa mitandao yote ya simu.

"Na mitandao yote imeunganishwa katika kulipia huduma hiyo, na maduhuli haya yamenza kukusanywa rasmi kuanzia Juni, 30 mwaka huu, na wakati mwaka wa fedha unafungwa tulikuwa tumeanza kukusanya kiasi cha sh milioni mbili,

"Lakini mpaka kufikia leo julai 2 kwa huu mwaka wa fedha 2024/25, ndani ya siku mbili tumeshakusanya zaidi ya sh milion 7, sasa tunaenda kutoa elimu kwa wanajamii wetu wa vijijini mkoani hapa na kuona jinsi gani maduhuli yataenda kuongezeka kama tulivyokusidia" amesema.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post