TAKUKURU DODOMA YAJIPANGA KUELIMISHA JAMII UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA



Na Dotto Kwilasa,Malunde Blog DODOMA

Tanzania ikiwa inajiandaa kuelekea kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa,taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa Mkoa wa Dodoma(TAKUKURU) imesema imejipanga kutoa elimu Kwa wananchi ili kupata viongozi bora.

Kamanda wa TAKUKURU Mkoani hapa John Joseph ameeleza kuwa wanatarajia kuanza kampeni hiyo ili kukomesha vitendo vya Rushwa hasa kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa nchini na kueleza kuwa moja ya mikakati waliojiwekea ni kuhakikisha wanatoa elimu kwa jamii ili kuwakumbusha madhara ya kupokea na kutoa rushwa.

Akizungumza hivi karibuni jijini Dodoma kwenye mkutano wake na waandishi wa habari amesema ,"baada ya kuwapatia semina ninyi waandishi tunaenda kwa wananchi na tutatoa semina kwa njia ya mikutano ya hadhara na tutapita maofisini kutoa semina pia kadri ya mda utakavyoruhusu hivyo tunatarajia kupata ushirikiano mkubwa sana kutoka kwa wananchi”amesema.

Aidha amesema kanuni za uchaguzi wa wenyeviti wa vijiji,wajumbe wa Halmashauri za vijiji na wenyeviti wa vitongoji katika mamlaka za wilaya ya mwaka 2019 imetoa utaratibu wa uchaguzi bila kujihusisha na vitendo vya Rushwa.

Ametaja sababu zinazopelekea kwenda kutoa elimu kwa wananchi dhidi ya vitendo vya rushwa hasa kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa ikiwa ni pamoja na jamii kurubiniwa kwa kupewa fedha ili kuchagua viongozi wasiofaa.

Amesema wamejipanga kutoa elimu katika maeneo mbalimbali jijini hapa ikiwa ni pamoja na kuandaa mikutano ya hadhara ili kuhakikisha kila mmoja anafikiwa na elimu hiyo.


Anasema wameamua kufanya hivyo ili kuhakikisha wanapatikana viongozi bora na kusaidia jamii nyingine ambayo Mara nyingi hurubuniwa,kitendo ambacho hakikubaliki kutokana na kwamba taifa linahitaji kupata viongozi bora na si bora kiongozi.


Kutokana na hayo baadhi ya Wananchi wametoa maoni yao na kusema suala la rushwa ni changamoto hivyo kuiomba TAKUKURU ifanye kazi ya kuelimisha jamii kuhusu kutoka kupokea rushwa wakati wa uchaguzi wa serikali za mitaa.


Grolia Lyimo anasema wakifanya hivyo itakuwa imewasaidia sana kupata viongozi Bora na si bora viongozi ambao watasaidia usimamizi wa maendeleo ikiwemo utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kueleza kuwa Suala la rushwa ni changanoto hivyo wananchi wanahaki ya kuelimishwa zaidi.


Anasema bila kufanya hivyo hawawezi kufika mbali na matokeo yake watapata viongozi wasiofaa.


Naye Hamis Juma alisema Jamii kubwa imekuwa ikirubuniwa na vitu vidogo na kushindwa kuchagua viongozi bora huku akiishukuru Takukuru kwa kiendelea kuielimisha Jamii huku akifafanua kuwa kwa kufanya hivyo itasaidia kuleta mabadiliko .


"Kazi kubwa hivi sasa Takukuru wanapaswa kuandaa mikutano ya hadhara ambayo itasaidia kuwaelimisha watu kuhusu rushwa,bado hawajachelewa,bado muda upo wa kutoa elimu Kwa wananchi ili kujua wanauwelewa kiasi gani kwenue masuala ya Rushwa, " amesema.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post