TVLA YATOA ELIMU KWENYE MAONESHO SABASABA


WATAALAM wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) wakiongozwa Mtendaji Mkuu wake Dkt. Stella Bitanyi wameendelea kutoa elimu kuhusiana na huduma mbalimbali zinazotolewa na TVLA katika Maonesho ya 48 ya Biashara Kimataifa ya Dar Es Salaam (Sabasaba) tangu yalipoanza Juni 28, 2024 na kutarajiwa kuhitimishwa Julai 13, 2024.

Akizungumza katika maonesho hayo Julai 05, 2024 Dkt. Bitanyi amesema kuwa katika Maonesho hayo TVLA imekuja kutangaza na kutoa elimu kuhusu huduma zinazotolewa na TVLA, ikiwemo umuhimu wa uchanjaji wa Mifugo, utambuzi wa magonjwa ya wanyama, uhakiki wa ubora wa vyakula vya Mifugo, utafiti wa magonjwa ya wanyama na ushauri kuhusu matumizi sahihi ya dawa za mifugo.

Aidha Dkt. Bitanyi aliongeza kuwa TVLA inatoa elimu ya udhibiti wa wadudu aina ya mbung’o pamoja na kuwadhibiti wadudu hao ambao hueneza ugonjwa wa Nagana.

Aliongeza kuwa TVLA inatoa elimu ya kudhibiti magonjwa yaenezwayo na kupe kama ndigana kali na ndigana baridi kwa kuhakiki ubora wa viuatilifu kwa ajili ya kuogesha wanyama ili kudhibiti kupe.

“Tunaendelea kuwakaribisha wananchi wote waliopo ndani ya viwanja vya maonyesho ya Sabasaba na maeneo mengine, kutembelea banda letu la TVLA lililopo kwenye banda la Wizara ya Mifugo na Uvuvi ili kupata elimu kuhusiana na udhibiti wa magojwa ya wanyama, chanjo za mifugo zinazozalishwa na TVLA, ufugaji pamoja na uhakiki wa ubora wa vyakula vya mifugo.” Alisema Dkt. Bitanyi.

Baadhi ya wadau wa Mifugo waliotembelea banda la TVLA wamefurahishwa na huduma zinazotolewa hasa elimu ya uchunguzi wa magonjwa ya Mifugo kabla ya kuwatibu pamoja na elimu ya uchanjaji wa Mifugo kwani walikuwa wanachanja Mifugo yao bili kuipima kitu ambacho kilikuwa kinasabasha vifo kwa Mifugo yao.

Maonesho ya 48 ya Biashara Kimataifa ya Dar Es Salaam (Sabasaba) yanayokutanisha wafugaji, wakulima, wafanyabishara na wajasiriamali kutoka kila pande za Dunia. TVLA imeshiriki kwa kuonesha teknolojia mbalimbali za kitaalamu na za kiubunifu.

Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Dkt. Stella Bitanyi (kushoto) akitoa elimu ya matumizi sahihi ya chanjo za Mifugo kwa raia wa kigeni waliotembelea banda la Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa ajili ya kujifunza namna bora za kuikinga Mifugo isishambuliwe na magonjwa Julai 5, 2024 kwenye maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar Es Salaam (Sabasaba).
Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Dkt. Stella Bitanyi (kushoto) akitoa elimu kwa mdau wa Mifugo kuhusiana uchunguzi wa magonjwa ya minyoo inayoathiri afya za Mifugo ili kuweza kuitambua na kushauri dawa zinaweza kutibu minyoo hiyo kwenye maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar Es Salaam (Sabasaba) Julai 05, 2024.
Mtaalam wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Bw. Denis Nyakilinga (kulia ) akitoa elimu kuhusiana na matumizi sahihi ya chanjo ya Homa ya Mapafu ya Ng’ombe kwa wanafunzi wa chuo cha Mifugo kilichopo kigamboni (Borigaram Agriculture Technical College) waliotembelea banda la Wizara ya Mifugo na uvuvi kujifunza shuguli za kimaabara zinazofanywa na TVLA kwenye maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar Es Salaam (Sabasaba) Julai 05, 2024.
Mtaalam wa Mifugo wa Wakala ya Maabara ya Veterinari (TVLA) Bw. Henri Mlundachuma akitoa elimu kwa mdau wa Mifugo alietembelea banda la Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuhusiana na uoteshaji wa vimelea vya bakteria (Media) kwa kutumia petri dishi kwa ajili ya kutambua dawa yenye ufanisi mzuri wa kutibu ugonjwa uliogundulika kwenye maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar Es Salaam (Sabasaba) Julai 05, 2024.
Matukio mbalimbali katika picha wataalam wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) wakitoa elimu kwa wadau wa Mifugo waliotembelea banda la Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupata elimu kuhusiana na shughuli mbalimbali zinazofanya na TVLA kwenye maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar Es Salaam (Sabasaba) Julai 05, 2024.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post