WAZIRI JAFO : KAMILISHENI JENGO LA VIWANDA NA BIASHARA KWA WAKATI


WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Dkt. Selemani Jafo akikagua ujenzi wa jengo la Wizara hiyo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma 

Na Mwandishi Wetu_DODOMA

WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Dkt. Selemani Jafo amekagua ujenzi wa jengo la Wizara hiyo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma na kuwataka wakandarasi kuhakikisha unakamilika kwa wakati.

Akizungumza Julai 8, 2024 baada ya kukagua ujenzi huo, Waziri Jafo ameridhishwa na kazi inayoendelea na matarajio ifikapo Septemba 30, 2024 ujenzi uwe umekamilika.

"Niwatake wasimamizi wa ujenzi huu ambayo ni Shirika la Nyumba Tanzania (NHC) wasimamie vizuri pamoja na mkandarasi kuhakikisha kazi unakamilika ndani ya muda uliopangwa, imani yetu itakapofika Septemba 30, 2024 sisi watumishi tuweze kuhamia kwenye jengo hili."

"Nimefarijika na mapokezi katika Wizara hii, jambo kubwa ambalo tumejiwekea malengo ni kuhakikisha mchakato wa majengo unakamilika katika hii awamu ya pili na watumishi wote wanahamia,"amesema.

Aidha amewataka watumishi wa Wizara hiyo kufanya kazi kwa bidii na ushirikiano.

"Ili tuweze kufikia Malengo ya Wizara yetu lazima tufanye kazi kwa bidii na Ushirikiano Ili tuendelee kumsaidia Rais wetu Mhe Dk.Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania", amesisitiza
WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Dkt. Selemani Jafo,akikagua ujenzi wa jengo la Wizara hiyo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.
WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Dkt. Selemani Jafo,akitoa Maelezo mara baada ya kukagua ujenzi wa jengo la Wizara hiyo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post