NI LAZIMA KILA MTOTO APATE CHAKULA SHULENI, WAZAZI WASIOCHANGIA WAFUATILIWE


Ofisa Elimu jiji la Tanga, Shomari Bane

Na Hamida Kamchalla, TANGA 

OFISA Elimu jiji la Tanga Shomari Bane ameagiza walimu wakuu wa shule za msingi jijini humo kuweka mkakati wa kuhakikisha suala la chakula linapewa kipaumbele kwa wanafunzi wote na ikibidi liwe la kisheria mashuleni humo.

Bane ameyasema hayo kwenye vikao vya hamasa kuhusu ujenzi kupitia miradi ya BOOST katika shule za msingi Kange iliyopo kata ya Mawezi na Ziwani iliyopo kata ya Pongwe ambavyo vilishirikisha watendaji wa Serikali za Mitaa pamoja na wananchi.

Amesema kila mtoto anapaswa kula chakula shuleni asubuhi na mchana ili waweze kuzingatia na kufaulu masomo yao ambapo pia amewataka wazazi kuchangia chakula hicho na kwa atakayekaidi kamati husika zimchukulie hatua.

"Ili tupate watoto bora katika masomo ni lazima kila mtoto apate chakula, na suala hili nitalifuatilia kwa ukaribu, walimu wakuu mnapaswa kuliweka kama sheria katika shule zenu" amesema Bane.

Lakini pia Bane amefafanua kuhusu suala la Elimu bila malipo kwamba hawana uelewa wa hilo wakidhani kwamba serikali ndiyo inahusika kwa kila kitu jambo ambalo wazazi wengi hawataki kuchangia hata chakula kwa watoto wao pindi walimu wanapotoa taarifa hiyo.

Amesisitiza kwamba serikali ya awamu ya tano iliyoongozwa na hayati Dkt. John Magufupi ilifuata sera ya kusaidia wazazi na kufuta michango ya hovyo hovyo shuleni na kufuta ada, kwa shule za msingi sh elfu moja, sekondari sh elfu 20 na sekondari ya upili sh elfu 70.

"Dhamira ya awamu ya tano ilikuwa ni kutoa ada na siyo kuendesha elimu bure, haipo Duniani kote hakuna nchi inayoendesha elimu bure, wananchi wanasema elimu bure na ndiyo maana hawataki hata kuchangia chakula cha mtoto, Mimi ndiyo nasimamia elimu katika jiji hili, tunasema (EBM), Elimu Bila Malipo",

"Kwa kuwa ninyi dhamira yenu ni kutesa watoto ndiyo maana naagiza watoto wale mashuleni kwa kuamini kwamba wazazi wengi muda hawakai majumbani, tunatarazaki kutafuta riziki, sasa basi tuchukue ile dhamira ya chakula cha mchana tukubaliane tunachanga kiasi gani" amesisitiza.

Sambamba na hilo Bane amesema wananchi wamepewa jukumu la kuchomba msingi na kufanya msalagambo wa wa kufikia kifusi, hivyo kutaka uongozi kuunda kamati kwa uwiano na kwamba nguvu zao linahitajika zaidi badala ya kutafuta mafundi.

Akizungumza mradi huo Mwenyekiti wa mtaa wa Kange Aidan Munisi amesema shule hiyo imepata kiasi cha sh milioni 88 na wananchi wameupokea na wako tayari kufanya kazi ambazo wameshirikishwa kujitokeza nguvu zao.

"Katika shule yetu na mtaa wetu mradi huu ni wa muhimu sana, fedha tulipatiwa za mradi wa BOOST tutahakikisha kwamba zinafanya kazi nzuri, wananchi wangu wako tayari kuchomba msingi na kusimamia shughuli za uchimbaji wa msingi hadi kushindilia zege" alisema.

"Tunajengewa vyumba vya madarasa vitatu na vyoo ambavyo vitajumuisha watu wenye ulemavu kwa wasichana na wavulana, wananchi wamelibeba hili na tunachosubiri ni mapimo kufanyika tuanze ujenzi ili watoto wetu wasome mahala pazuri" amebainisha.

Naye diwani wa Maweni Joseph Colyvas amesema shule hiyo ni ya zamani na ina majengo mengi chakavu lakini kwa mradi huo wana imani hata mandhari yake yatakwenda kubadilika na kwamba wako wameupokea na wako tayari kwa utekelezaji.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post