KAMATI YAPONGEZA WIZARA KATIKA ULINZI NA USALAMA WA MTOTO


Na WMJJWM-Dodoma

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Maendeleo na Ustawi wa Jamii imeipongeza Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa kuweka Mpango mkakati wa kuwalinda watoto Kisheria dhidi ya mabadiliko yanayotokana na sayansi na Teknolojia duniani.
Hayo yamebainika wakati Wizara ikiwasilishaji maelezo kuhusu marekebisho ya Sheria zinazuhusu ulinzi wa mtoto nchini mbele ya Kamati hiyo Jijini Dodoma (Agosti 17, 2024)

Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Fatma Toufiq amesema marekebisho hayo ni muhimu kwa Ustawi wa watoto na yatasaidia kwenda na wakati ikiwa ni pamoja na kumlinda mtoto dhidi ya vitendo vya ukatili.

"Mimi niwapongeze mswaada wa marekebisho ya Sheria zinazohusu ulinzi watoto ni mwanga na mwanzo mzuri wa kuandaa mazingira salama kwa watoto wetu katika malezi na kumlinda dhidi ya vitendo vya ukatili" amesema Mhe. Fatma
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Mwanaidi Ali Khamis amesema Wizara imeona umuhimu wa kufanyika marekebisho ya Sheria zinazohusu ulinzi wa mtoto kutokana na masuala mbalimbali ikiwemo mijadala ya wabunge na wadau wa maendeleo ya Mtoto.

"Sisi Wizara tutaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa ulinzi wa mtoto ili kuhakisha Tanzania inakuwa mahali salama kwa Mtoto katika hatua zote za Makuzi yake"amesema Mhe. Mwanaidi

Akiwasilisha hoja za marekebisho ya Sheria zinazohusu ulinzi wa mtoto nchini, Mkurugenzi wa Huduma za Sheria kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Evelyn Makala amesema Wizara imepewa dhamana ya kusimamia ulinzi na usalama wa mtoto nchini kwa kutumia mifumo ya kitaasisi, kisera na Kisheria.

Amesema Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 ni nguzo muhimu ambayo imetoa haki kwa Mtoto ikisaidiwa na Sheria mbalimbali zenye kumlinda mtoto kwa kutoa adhabu stahiki kutokana ukiukwaji Sheria hizo ikiwemo adhabu ya miaka 30 kwa wale wanaobainika kuvunja sheria.

"Katika kuona changamoto mbalimbali kwenye Sheria zilizopo ikiwemo maendeleo ya sayansi na teknolojia na masuala mengine imesababisha Serikali kupitia Wizara yetu kuja na marekebisho ya Sheria zinazuhusu ulinzi wa mtoto" amesema Evelyn.

Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalum iko katika hatua ya kupeleka muswada wa marekebisho ya Sheria zinazohusu ulinzi wa mtoto mwaka 2024 kwa lengo la kuhakikisha watoto wanalindwa na kuepushwa na vitendo vyote vya ukatili.




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post