SERA YA VIJANA YAZINDULIWA DODOMA



Na Dotto Kwilasa, Dodoma

Hatimaye Sera mpya ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ya mwaka 2007 toleo la 2024 imezinduliwa rasmi Dodoma huku kukiwa na matarajio makubwa ya kujibu changamoto za vijana .
Aidha sera hiyo inatazamwa kama mwanga na mwongozo wa kuanzishwa rasmi kwa Baraza la Taifa la Vijana.

Hayo yamebainishwa leo Agosti 12,2024 jijini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi,Vijana, Ajira na Watu wenye ulemavu,Mhe. Ridiwani Kikwete, wakati akizungumza kwenye maadhimisho ya siku ya vijana kimataifa.

Amesema,Serikali imekwisha kamilisha mapitio ya Sera ya Taifa ya Vijana ya mwaka 2007 na marekebisho yake imefanyiwa mwaka 2024 na leo hii tunakwenda kuizindua muda mfupi ujao.

Amesema changamoto nyingi zinazoelezwa kwa vijana zinatokana na ukweli kwamba yako baadhi ya maeneo hayana miongozo yake kupitia sera hii ya vijana ambayo tutaizundua leo nina hakika kabisa vilio vya vijana wengi vinakwenda kupataiwa ufumbuzi baada ya kupitishwa kwa sera .

Aidha, amesema kuwa sera hiyo inaeleza uelekeo na njia ambazo wanakwenda kuzitumia kwa pamoja ili kufikia malengo ambayo yanatatua matatizo waliyonayo vijana.

“Sera hii inakwenda kuanzisha baraza la taifa la vijana uanzishaji wa baraza hili la vijana unakwenda kuwa muarobani wa kutambua na kutatua changamoto nyingi za vijana.

“Vijana wamekosa maeneo ya kueleza changamoto zao vijana walikosa watu wa kuwasikiliza, vijana walikosa msukumo wa kufikisha changamoto zao na kuzitafutia majawabu kwa pamoja”amesema Mhe.Ridhiwan.

Amesema, ujio wa sera hiyo ya vijana na uudwaji wa baraza la taifa la vijana unaonesha wazi azma ya Rais Samia kujidhatiti na changamoto zote zinazo wakabili vijana zinapatiwa majibu.

Hata hivyo amesema kuwa sera hiyo pia inakwenda kutambua vijana katika sekta zote wanaofanya kazi katika maeneo hatarishi ikiwemo ya madini, maeneo ya uzalishaji mali ikiwemo mashambani na kwenye mifugo.

“Wapo vijana wanaofanya kazi za sanaa ikiwemo wabunifu, muziki, michezo, ubunifu na utungaji wa sanaa mbalimbali sera hii inakwenda katika maeneo hayo.

Pia ametoa wito kwa maafisa kazi kutambua kuwa nafasi zao siyo za kukaa ofisini wakisubiri vijana waje kulia na kueleza changamoto zao.

Kwa upande wake Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu(Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Bi. Mary Maganga,amesema katika kuadhimisha siku ya vijana, wameendesha kongamano la siku mbili lililokutanisha vijana zaidi ya 3,000 kutoka maeneo mbalimbali ya Tanzania.

“Katika kongamano hilo, vijana wamechangia juu ya mada za Sera ya Maendeleo ya 2050, fursa za kidigitali, vijana na uchumi, afya ya akili na saikolojia ya vijana na kusisitiza kuwa serikali imechukua maoni ya vijana katika eneo la elimu, afya, ajira na uwezeshaji.”amesema Bi.Maganga

Naye Mwakilishi wa Vijana, Charles Ruben amempongeza Rais Samia kwa jitihada zake kuwainua na kuwasaidia vijana wa kitanzania na kuwa vijana wamepata elimu na ujuzi wa kazi unaofanya vijana kushiriki katika shughuli za kiuchumi na kuwapo ongezeko la vijana kwenye uongozi.

“Ajira za vijana zimeongezeka ambapo kuanzia mwaka 2023 hadi 2024 ajira 607675 zimezalishwa huku ajira 204,000 zikitokana na miradi ya kimkakati inayotekelezwa hapa nchini huku akitenga Sh bilioni 1.1 kwa ajili ya miradi ya jenga kesho iliyobora BBT ambayo inawalenga vijana.”amesema 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post