TCB YAINGIA MKATABA WA MAKUBALIANO NA ZEEA KUWEZESHA MIKOPO KWA WANAWAKE NA VIJANA


Benki ya Biashara Tanzania (TCB) imesaini Mkataba wa makubaliano (MOU) na Wakala wa Serikali wa Uwezeshaji Wananchi kiuchumi Zanzibar ( ZEEA) kuanzisha mpango maalumu wa mikopo utakaonufaisha makundi maalum wakiwemo wanawake na vijana wanaojihusisha na shughuli za kiuchumi visiwani Zanzibar.

Mpango huo unakusudia kuchochea ukuaji wa biashara, ongezeko la ajira, na maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika leo Agosti 2,2024 Jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu Afisa ya Rais ( Kazi na Uwezeshaji ), Maryam Juma Abdulla amesema tayari shilingi bilioni 2 zimeshakusanywa na halmashauri visiwani humo ili kuanza uwezeshaji.

Aidha ameitaka benki ya TCB kuhakikisha inafanya tathmini ya mikopo wanayotoa kwa makundi hayo ili ziweze kurejeshwa kwa wakati na wengine waweze kukopa .

"Programu hii inakwenda kuwagusa wanawake, vijana na walemavu na tayari yameshaletwa maombi 34 ambapo 19 ni maombi rasmi yanayotoka kwa vikundi vya wanawake, 13 kwa vijana na 2 kutoka kwa watu wenye ulemavu" amesema

Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa TCB, Adam Mihayo amesema Mkataba huu wa makubaliano unathibitisha dhamira ya Benki ya TCB kuwezesha uchumi jumuishi na maendeleo ya kiuchumi kwa ujumla.

"Mpango huu unaendana na lengo letu la kuwezesha maendeleo ya kiuchumi kwa kujenga uchumi jumuishi. Kwa kuyawezesha makundi maalum, tunaziinua biashara binafsi, pamoja nakuimarisha mfumo mzima wa uchumi na kutengeneza mazingira imara ya kiuchumi"amesema Mihayo

Ameongeza kuwa Mpango huo wa mikopo umekusudiwa kutia chachu juhudi za kijasiriamali, kuwapa wajasiriamali uthubutu wa kuanzisha na kupanua biashara zao n a Malengo ya uwezeshaji huu ni kuwa chanzo cha mabadiliko mengine kama kuimarisha biashara na uchumi.

Nae Mkurugenzi Mtendaji wa ZEEA, Juma Burhan Mohamed amesema wanalenga kuipatia benki ya TCb kiasi cha shilingi bilioni 1.8 ili waanze utoaji wa mikopo hiyo ambayo itarejeshwa kwa kipindi cha miaka 2.

"Lengo la mikopo hiyo kiwa ni kuvifikia vikundi 75 vyenye wanachama kati ya watano (5) mpaka ishirini (20), ZEEA mpaka sasa imeshasajili vikundi 16 kutoka sekta mtambuka na kupokea maombi ya mkopo yanayofikia wastani wa shilingi milioni 150"amesema Mohamed.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post