WAKUU WA WILAYA NA WAKURUGENZI NDANI YA MKOA WA SHINYANGA, HAKIKISHENI MASOKO YOTE YANAKUWA SAFI WAKATI WOTE - RC MACHA


MKUU wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Anamringi Macha amewaagiza Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wote ndani ya Mkoa wa Shinyanga kuhakikisha kuwa masoko na magulio yote yanafanyiwa usafi na kuwa safi wakati wote kwa kuwa kwa sehemu kubwa ndiyo kunapatikana vyakula ambavyo tunakula lakini pia kwa sehemu kubwa ndiyo kwenye mkusanyiko wa watu wengi zaidi.

RC Macha ameyasema haya leo tarehe 20 Septemba, 2024 wakati alipoongoza wananchi wa Mkoa wa Shinyanga kusafisha mazingira katika soko la Nguzonane lililopo Manispaa ya Shinyanga ikiwa ni Maadhimisho ya Siku ya Usafishaji Duniani ambapo kwa Mkoa wa Shinyanga yamefanyika hapa Manispaa ya Shinyanga. 

"Nitumie nafasi hii kuwaagiza Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wote ndani ya Mkoa wa Shinyanga kuhakikisha kuwa masoko na magulio yote katika maeneo yao yanafanyiwa usafi na kuwa safi wakati wote kwakuwa kwa sehemu kubwa ndiyo maeneo ambayo chakula kinapatikana na ndiyo kwenye mkusanyiko wa watu wengi zaidi," amesema RC Macha.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga CP. Salum Hamduni ambaye ameongoza watumishi wengine wote, Taasisi, Vyombo vya Usalama na wadau wa usafi mkoani Shinyanya amesema kuwa Siku ya usafishaji Duniani (WORLD CLENAUP DAY) chimbuko lake ni huko ESTONIA iliyopo Ulaya Kaskazini ambapo asilimia 4 ya watu walijitokeza pasipo shuruti ya serikali kufanya usafi wa mazingira nchi nzima kwa masaa kadhaa tu, jambo hili lileta muamko na mvuto wa kipekee kwa jamii nzima na serikali, likapata kibali sana, wakati huo liliongozwa na kauli mbiu “NCHI MOJA, SIKU MOJA”. 

"Jambo hili halikubaki kuwa siri tena kwa watu wa Estonia tu bali lilileta muamko wa kihisia na kupokelewa na jamii mbalimbali Duniani kwa kuja na msemo wa “DUNIA, TUFANYE” (Let’s Do it! World), na hapo jambo likaunganisha watu kutoka pande zote za Dunia na kuamua kuwa na siku maalumu ya usafi ambayo ni tarehe 20 septemba. Siku hii haijabaki kama siku ya kuondoa taka ngumu tu bali ni siku ya kimkakati wa kutokomeza magonjwa ya mlipuko yanayotokana na uchafu na kwa Tanzania maadhimisho haya yameanza kuadhimishwa kwa mara ya kwanza mwaka 2018 na kuanzia hapo kila ifikapo tarehe 20 Septemba kama leo huwa ni maadhimisho yake," amesema RAS CP. Hamduni.

Usafi ni suala nyeti linalomgusa kila mtu. Usafi unayagusa maisha yetu ya kila siku, mbali na kwamba ni ustaarabu lakini linachangia kwa kiasi kikubwa kupunguza magonjwa ya kuambukiza na mlipuko yanayotokana na uchafu wa mazingira kama vile Magonjwa ya mfumo wa upumuaji, Kuhara damu, Minyoo, Malaria n.k.

Kauli mbiu ya maadhimisho haya inasema "Uhai Hauna Mbadala, Zingatia Usafi wa Mazingira".























Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post