RAIS SAMIA : SERIKALI INAENDELEA KUIMARISHA UPATIKANAJI WA UMEME NCHINI

 

📌 Lengo ni kuimarisha upatikanaji wa umeme
📌 Asema njia ya umeme Songea - Tunduru itaiunganisha Mikoa ya Lindi na Mtwara na gridi ya Taifa
📌 Vijiji 541 vyafikiwa na huduma ya umeme kati ya Vijiji 551 mkoani Ruvuma
📌 Asisitiza hakuna mwananchi aliyepisha mradi ambaye hata lipwa fidia


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema Serikali inaendelea kuimarisha upatikanaji wa umeme nchini ambapo inatekeleza mradi wa ujenzi wa kituo cha kupokea umeme cha Tunduru ambacho utekelezaji wake umefikia asilimia 50.


Rais Samia ameyasema hayo leo Septemba 28, 2024 wakati akihitimisha ziara yake mkoani Ruvuma iliyokuwa na lengo la kujipima ni kwa kiasi gani Serikali imeweza kutekeleza ahadi ilizo zitoa kwa wananchi.


"Ndugu zangu kukamilika kwa mradi huu pamoja na kuunufaisha Mkoa wa Ruvuma lakini pia utapelekea kuiunganisha Mikoa ya Lindi na Mtwara kuiwezesha kupata umeme wa gridi ya Taifa." Amesema Rais Samia.


Ameongeza kuwa, Serikali inafanya juhudi kubwa katika kusogeza huduma za umeme kwenye kila kijiji ambapo Serikali kupitia REA imefikisha umeme kwenye Vijiji 541 kati ya Vijiji 551 vya Mkoa wa Ruvuma na kuongeza kuwa Serikali inaendelea kusogeza huduma kwenye vitongoji mkoani humo.


Aidha, ametoa wito kwa wananchi ambao bado hawajalipwa fidia ili kupisha utekelezaji wa miradi ya umeme, kupisha utekelezaji kwani Serikali italipa fidia zao na kuongeza kuwa hakuna mwananchi ambaye hata lipwa fidia.


Pia, ametoa wito kwa viongozi wa Serikali na watumishi wa wananchi kuendelea kutoa elimu ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kuokoa maisha ya watanzania pamoja na misitu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post