UZINDUZI TAMASHA LA UTAMADUNI WAITEKA RUVUMA


Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Dk. Damas Ndumbaro pamoja na viongozi wengine wakitoa burudani staili ya Misomisondo mara baada ya kufungua Tamasha la tatu la utamaduni la Kitaifa mkoani Ruvuma Septemba 20, 2024 katika Uwanja wa Majimaji Manispaa ya Songea.

Na Mwandishi Wetu, RUVUMA

WAZIRI wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Damas Ndumbaro amewaasa watanzania kuzingatia miiko, mila na desturi za kitanzania na kuwarithisha watoto na vijana ili kujiepusha na tamaduni za kigeni zisizofaa kwa jamii.

Aidha, ameitaka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuwachukulia hatua kale wale wale wanaoua mila na desturi za watanzania kwenye mitandao ya kijamii.

Akizindua Tamasha la tatu la Utamaduni Kitaifa kwenye uwanja wa Majimaji mjini Songea, alisema kusipokuwa na utamaduni hakutakuwa na utu na wasipouenzi hawatauendeleza.

“Ili Taifa liwe hai lazima tuenzi na kuendeleza utamaduni wetu, na lazima turithishe utamaduni wetu kwa vijana na watoto na lazima tuwafundishe watoto wetu mil ana desturi za kitanzania, Kiswahili tuwafundishe miiko mbalimbali na historia yetu kwa kuwa hawa watoto ni taifa la kesho,”alisema.

Alisema katika maadhimisho ya tamasha hilo ilitolewa semina ya maadili na utamaduni iliyofundisha jinsi ya kuenzi utamaduni na namna ya kukabiliana na madhara ya sayansi na teknolojia katika kulinda, kuenzi na kuendeleza mil ana desturi.

“Sasa hivi duniani kuna suala linaitwa haki za binadamu ni jambo linalopaswa kuliheshimu na kulizingatia lakini tusitumie haki za binadamu kuingiza tamaduni za kigeni zisizofaa katika jamii yetu,”alisema.

Alisema wakifanya hivyo wataua nchi na itakuwa mfu.

“Taasisi za elimu kuanzia chekechea hadi chuo kikuu ni muhimu kurithisha utamaduni wet una mila zetu katika kupambana na mmonyoko wa maadili,”alisema.

Alikemea tabia ya familia kulaumu mmonyoko wa maadili badala ya kujikita kutoa elimu kwa watoto na vijana ili kuishi kwenye tamaduni za mtanzania.

Hata hivyo, alisema taasisi za dini zina nafasi ya kukabiliana na mmonyoko wa maadili na kurithisha utamaduni kwa watoto na vijana.

“Tuwafundishe maadili mema watoto wetu, viongozi wa dini mna kazi kubwa sana na maadili mengi ya dini yanatusaidia kulinda tamaduni zetu,”alisema.

Awali, Dk.Ndumbaro alibainisha kuwa Septemba 8, 2021 katika maadhimisho ya utamaduni Bujora mkoani Mwanza Rais Samia Hassan Suluhu alitoa maelekezo kwa Wizara hiyo kuandaa tamasha la kitaifa litakalofanyika kila mkoa.

“Maelekezo yale yametufanya tuwe Songea leo, uwepo wetu hapa ni maelekezo ya Rais Samia kudumisha tamaduni zetu, ”alisema.

Alisema Tanzania imebarikiwa kuwa na makabila zaidi ya 120 na lugha za kijamii zaidi ya 150 na ni utajiri wa kiutamaduni.

“Utamaduni wetu unategemea nguzo zifuatazo moja ni upendo, mshikamano, umoja, amani na utulivu, yote tunayoyafanya ili kuendeleza nguzo hizi,”alisema.

Waziri Ndumbaro alisema Tamasha hilo lina umuhimu mkubwa na ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM Mwaka 2020-2025 ambayo imeagiza Wizara yenye dhamana ya utamaduni Sanaa na michezo kuhakikisha inaenzi, kukuza na kuendeleza utamaduni wa mtanzania.

Alisema tamasha hilo linasaidia kukuza utalii wa utamaduni na kuvutia watu nje ya mipaka ya Tanzania.

“Tamasha hili kilele chake ni Septemba 23, 2024 na mgeni rasmi ni Chifu Hangaya Rais Samia kwenye viwanja hivi kuanzia saa 12 asubuhi mageti yatakuwa wazi, jitokezeni kwa wingi tudumishe tamaduni zetu,”alisema.

Alisema kutakuwa na mashindano ya ngoma kutoka Tanzania Bara na Zanzibar sambamba na maonesho ya utamaduni na vyakula vya asili.

“Kesho (leo)kutakuwa na onesho la kanga ni utamaduni wa kitanzania na inamaana sana kwenye utamaduni wetu, mtoto akizaliwa anapokelewa na kanga, msibani wanawake wanavaa kanga, msikitini wanavaa kanga, shambani wanavaa kanga, wanaume pia tunavaa kanga na akivaa ina tafsiri nyingi kwamba huyo mume wa mtu usimguse. Mgeni rasmi ni Mkuu wa Mkoa wa Songwe Daniel Chongolo,”alisema.

Pamoja na hayo, alisema baada ya kilele hicho Rais Samia atakuwa na ziara ya kikazi mkoani Ruvuma na kuhamasisha wananchi wajitokeze kwa wingi kwenye ziara hiyo itakayoambatana na ukaguzi wa miradi ya maendeleo.

UCHAGUZI WA SERIKALI ZA MITAA Waziri Ndumbaro aliwakumbusha wananchi kushiriki ipasavyo kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa kwa kuwa maendeleo yote yanaanzisha kwenye ngazi ya mitaa.

“Watanzania tujitokeze kujiandikisha na kuboresha taarifa zetu kwenye daftari la mpigakura kwa kuwa kupiga kura ni haki ya msingi na kikatiba, na tujitokeze kuchukua fomu kugombea nafasi mbalimbali ili kupata viongozi wa kuenzi na kuendeleza nchi yetu ngazi ya serikali za mitaa,”alisema.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Kanali Ahmed Abbas Ahmed, alisema Ruvuma bado inaongoza kwenye utamaduni na kwamba viongozi wanatambua umuhimu mkubwa wa kukuza tamaduni, Sanaa na michezo nchini .

Aliwaomba wageni kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo mkoani humo.

Awali, Katibu wa Machifu Tanzania, Nyamilonda Mikomangwa, alisema umoja wa machifu unampongeza Rais Samia kwa kuona umuhimu wa kuenzi utamaduni wa watanzania.

“Machifu wote tutakuwa hapa kufurahia tamasha zuri la kuenzi utamaduni wetu na milana desturi za mtanzania,”alisema.



WAZIRI wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Damas Ndumbaro,akizungumza wakati akizindua Tamasha la tatu la Utamaduni Kitaifa kwenye uwanja wa Majimaji mjini Songea,leo Septemba 20,2024.





Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamis Mwinjuma maarufu Mwana FA,akizungumza wakati wa uzinduzi wa Tamasha la tatu la Utamaduni Kitaifa kwenye uwanja wa Majimaji mjini Songea,leo Septemba 20,2024.





MKUU wa Mkoa wa Ruvuma, Kanali Ahmed Abbas Ahmed,akizungumza wakati wa uzinduzi wa Tamasha la tatu la Utamaduni Kitaifa kwenye uwanja wa Majimaji mjini Songea,leo Septemba 20,2024.



Katibu wa Machifu Tanzania, Nyamilonda Mikomangwa,akizungumza wakati wa uzinduzi wa Tamasha la tatu la Utamaduni Kitaifa kwenye uwanja wa Majimaji mjini Songea,leo Septemba 20,2024.





Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Dk. Damas Ndumbaro pamoja na viongozi wengine wakitoa burudani staili ya Misomisondo mara baada ya kufungua Tamasha la tatu la utamaduni la Kitaifa mkoani Ruvuma Septemba 20, 2024 katika Uwanja wa Majimaji Manispaa ya Songea.



SEHEMU ya wananchi wakisikiliza hotuba ya Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Damas Ndumbaro (hayupo pichani),akizungumza wakati akizindua Tamasha la tatu la Utamaduni Kitaifa kwenye uwanja wa Majimaji mjini Songea,leo Septemba 20,2024.



Vikundi vya ngoma za asili vikitoa burudani kwenye ufunguzi wa Tamasha la tatu la utamaduni la Kitaifa mkoani Ruvuma Septemba 20, 2024 katika Uwanja wa Majimaji Manispaa ya Songea.



Vikundi vya ngoma za asili vikitoa burudani kwenye ufunguzi wa Tamasha la tatu la utamaduni la Kitaifa mkoani Ruvuma Septemba 20, 2024 katika Uwanja wa Majimaji Manispaa ya Songea.



Vikundi vya ngoma za asili vikitoa burudani kwenye ufunguzi wa Tamasha la tatu la utamaduni la Kitaifa mkoani Ruvuma Septemba 20, 2024 katika Uwanja wa Majimaji Manispaa ya Songea.



Vikundi vya ngoma za asili vikitoa burudani kwenye ufunguzi wa Tamasha la tatu la utamaduni la Kitaifa mkoani Ruvuma Septemba 20, 2024 katika Uwanja wa Majimaji Manispaa ya Songea.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post