TATCA YAADHIMISHA SIKU YA KIMATAIFA YA MUONGOZA NDEGE KWA KUTOA ELIMU KWA WANAFUNZI WA SKULI YA LUMUMBA ZANZIBAR


Chama cha Waongoza Ndege Tanzania (TATCA), kimeadhimisha siku ya kimataifa ya muongoza ndege duniani kwa kutoa elimu kuhusu kazi za kuongoza ndege kwa wanafunzi wa Skuli ya Lumumba iliyopo Zanzibar.

Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo yaliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Jengo la Tatu la Abiria katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume (AAKIA), rais wa TATCA Bw. Merkiory Ndaboya aliwataka wanafunzi hao kuweka bidii ili waweze kujiunga na fani hiyo hapo baadae.

Awali Bw.Ndaboya aliwaeleza wanafunzi hao historia ya taaluma ya Uongozaji ndege nchini na duniani kwa ujumla.

Mbali na wanafunzi hao, TATCA pia ilialika wadau wa Usafiri wa Anga kutoka Zanzibar, ambao kwa pamoja walipata uelewa juu ya majukumu ya taaluma hiyo, changamoto pamoja na muelekeo hasa katika ukuaji wa teknolojia.

Kwa upande wake, Meneja wa TCAA kituo cha Uwanja wa Ndege wa AAKIA Bw. Mohamed Ali Mohamed alitoa wito kwa wadau wote kuungana na Waongoza Ndege wa Tanzania kuadhimisha siku hiyo muhimu na kuainisha usalama wa usafiri wa anga ni jukumu la wadau wote.

"Na mfahamu kuwa leo siku hii inaadhimishwa kwa mwaka wa 101, taaluma hii ina nafasi kubwa sana katika kuendelea kukuza uchumi wa Taifa letu na hasa sekta ya utalii kwani kwa asilimia kubwa watalii wanakuja na kuondoka nchini kwa kutumia Usafiri wa Anga," alisema Bw. Mohamed.

Aidha, mbali na mafunzo yaliyotolewa kupitia mawasilisho na majadiliano, wanafunzi na wadau waliohudhuria hafla hiyo walipata wasaa wa kutembelea ofisi ya TCAA uwanjani hapo na kujionea shughuli mbalimbal ikiwemo na Uongozaji wa Ndege.

Walimu na wanafunzi hao kutoka Skuli ya Lumumba walionesha kufurahishwa na namna siku hiyo ilivyoadhimishwa na kuishukuru TCAA kupitia TATCA kwa mualiko na elimu waliyoipata.

Siku hiyo ilihitimishwa kwa kutembelea kituo cha kulea watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu cha Mazizini.

Afisa Muongozaji Ndege Mkuu Kituo Cha TCAA Uwanja wa Ndege wa AAKIA Abdalah Suleiman akitoa maelezo kwa wanafunzi wa Skuli ya Lumumba walipotembelea Mnara wa Kuongozea Ndege wakati wa Maadhimisho ya siku ya kimataifa ya muongoza ndege duniani.
Rais wa Chama cha Waongoza Ndege Tanzania (TATCA) Merikiory Ndaboya akizungumza na wanafunzi wa Skuli ya Lumumba kuhusu namna wanavyoweza kufikia marengo hasa kuingia kwenye fani ya Uongozaji ndege wakati wa Maadhimisho ya siku ya kimataifa ya muongoza ndege duniani yaliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Jengo la Tatu la Abiria katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume (AAKIA),
Meneja wa TCAA kituo cha Uwanja wa Ndege wa AAKIA Bw. Mohamed Ali Mohamed akizungumza na wanafunzi wa Skuli ya Lumumba kuhusu umuhimu wa fani hii wakati wa Maadhimisho ya siku ya kimataifa ya muongoza ndege duniani.
Afisa Muongozaji Ndege Mstaafu Ambaye pia aliwahi Kuwa Meneja wa TCAA Zanzibar Said Sumry akiwahamasisha wanafunzi kusoma fani ya uongozaji ndege wakati wa Maadhimisho ya siku ya kimataifa ya muongoza ndege duniani yaliyofanyika
Baadhi ya wanafunzi wa skuli ya Lumumba wakisikiliza mada zilizokuwa zinatolewa wakati wa Maadhimisho ya siku ya kimataifa ya muongoza ndege duniani.
Picha ya pamoja

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post